Sunday, May 22, 2016

MADIWANI NAMTUMBO WAILALAMIKIA KAMPUNI YA MANTRA KWA KUTOTOA USHIRIKIANO KWA HALMASHAURI

Baadhi ya Waandishi wa habari mkoa wa Ruvuma, ambao walitembelea Kampuni ya Mantra inayotarajia kuanza kuchimba madini aina ya Urani wilayani Namtumbo mkoani humo, wakipata ufafanuzi juu ya madini hayo kutoka kwa Wataalamu wa kampuni hiyo.


Na Steven Augustino,
Namtumbo.

KAMPUNI ya Mantra inayotarajia kuchimba madini ya Urani,  katika  eneo  la  mto Mkuju wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma imetuhumiwa kwamba imekuwa haitoi ushirikiano kwa Halmashauri ya wilaya hiyo, pale wanapoalikwa kuhudhuria mikutano ya baraza  la Madiwani wilayani humo.

Tuhuma hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa baraza hilo, Daniel Nyambo mbele ya Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Ally Mpenye wakati akizungumza na Madiwani hao katika kikao cha baraza  hilo kilichoketi hivi  karibuni wilayani humo.

Wakifafanua taarifa hiyo kwa nyakati tofauti, Nyambo na Mkurugenzi wa  Halmashauri  hiyo, Ally Mpenye waliwaeleza Madiwani hao kwamba kila wanapowalika viongozi wa kampuni hiyo kwa ajili ya kuhudhuria  vikao  vya  baraza hilo, hawafiki jambo linalowaletea mashaka juu ya mambo wanayotaka kuficha wakati wa utekelezaji wa mradi huo na madhara yanayoweza kujitokeza kwa jamii.


Aidha walibainisha kuwa mialiko wanayoitoa kwa kampuni hiyo kuhudhuria  vikao vya baraza hilo, ili waweze kutoa elimu kuhusu madini  hayo kwa  Madiwani  wamekuwa hawaonekani licha ya kampuni ya Mantra, kuisaidia Halmashauri  katika baadhi  ya mambo pale inapoombwa kufanya hivyo.

Kufuatia hali hiyo Madiwani hao waliwataka Mwenyekiti na Mkurugenzi wa Halmashauri  ya wilaya ya Namtumbo, kuendelea  kuuomba uongozi  wa kampuni  hiyo kutoa  elimu kuhusu madini  hayo  ili na wao wakatoe  elimu kwa wananchi  wao, juu ya madhara yanayoweza kujitokeza wakati wa utekelezaji wa mradi huo.

Katika kutaka kujiridhisha juu ya tuhuma hizo, mwandishi  wetu alikwenda katika  Ofisi za mahusiano ya jamii ya kampuni  ya Mantra iliyopo mjini Namtumbo ambapo  alikutana na mlinzi wa ofisi hiyo na kuambiwa kuwa,  Afisa mahusiano huyo ambaye alimtaja kwa jina la Khadija  Pallangyo ambaye alidai kuwa siku zote hukaa Songea mjini na  kwamba, hufika ofisini hapo pindi anapokuwa na  kazi ya  kufanya.

Hata hivyo Afisa mahusiano huyo Pallangyo alipotafutwa kuzungumzia  malalamiko  hayo ya Madiwani, ambao walidai kuwa kutopatikana kwa maafisa hao kumewafanya washindwe kutekeleza mipango yao ya kutoa elimu kwa umma, kutokana na uongozi wa Mantra kutohudhuria vikao hivyo vya baraza la Madiwani kila wanapoombwa kufanya hivyo.

No comments: