Saturday, May 7, 2016

KAMPUNI YA OVANS YAWEKA MIKAKATI YA VIJANA KUEPUKANA NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

VIJANA wanaojishughulisha na kazi ya ufyatuaji tofari za udongo katika mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, wameshauriwa kujiunga na Kampuni ya Ovans Construction Limited ili waweze kufanya kazi hiyo kwa kutumia mashine ya kisasa ya kufyatua tofari za kuchanganya mchanga na simenti, ikiwa ni lengo la kuepukana na uharibifu wa mazingira katika mji huo.

Uhamasishaji huo wa vijana kuachana na kazi ya ufyatuaji wa tofari za udongo ambao hufanywa mabondeni, ni njia ya kuepukana pia na uharibifu wa vyanzo vya maji ambao unaendelea kushika kasi kila siku katika mji huo.

Valence Urio.
Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Valence Urio alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ambapo alifafanua kuwa kazi hiyo ya uundaji wa tofari za udongo pia huchangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa misitu, ambapo wafyatuaji hulazimika kukata miti msituni kwa ajili ya kuweza kupata kuni za kuchomea tofari.

Valence alisema kuwa baada ya kuona uharibifu huo wa mazingira ukiwa unaendelea katika mji huo aliona ni vyema anunue mashine ya kisasa ambayo itaweza kufanya kazi ya kufyatua tofari za kuchanganya mchanga na simenti, na kuwataka vijana wanaojishughulisha na kazi hiyo wajikusanye kwa pamoja na yeye atawasaidia kuunda kikundi ambacho kitasajiliwa kisheria na kuweza kufanya kazi hiyo ya kuwaletea kipato.


“Ninahamasisha vijana wote hapa Mbinga waje kufanya kazi hii, lengo waachane na kazi ya ufyatuaji tofari za udongo mabondeni kwani huchangia kuharibu mazingira yetu, vilevile kampuni inahamasisha upandaji wa miti rafiki ya maji kwenye vyanzo vyetu vya maji”, alisema Valence.

Alisema mashine hiyo ambayo ujenzi wake umekwisha anza, anatarajia ifikapo Mei 10 mwaka huu kazi rasmi ya ufyatuaji wa tofari hizo za simenti (blocks) utaanza na kwamba tofari moja litakuwa linauzwa kwa shilingi 1,000.


Mkurugenzi huyo wa Ovans Construction Limited aliongeza kuwa, kampuni hiyo pia imeweza kusaidia vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga kuanzisha mradi wa ushonaji nguo na husimamia mikopo benki ya kikundi cha vijana, kinachofahamika kwa jina la ‘Kusile waendesha boda boda’ kilichopo mjini hapa ili waweze kujipatia kipato na kusukuma mbele gurudumu la maendeleo katika maisha yao.

No comments: