Thursday, May 5, 2016

GAMA SONGEA ATOA MSAADA WA MAGARI YAKUWAHUDUMIA WANANCHI WAKE

Na Julius Konala,
Songea.

MBUNGE wa Jimbo la Songea mjini mkoani Ruvuma, Leonidas Gama ametoa msaada wa magari mawili ikiwemo la kubebea wagonjwa kwa ajili ya kusaidia wananchi wa jimbo hilo kwenda hospitali, pale wanapougua au kuzidiwa na magonjwa mbalimbali.

Msaada huo ulitolewa na Mbunge huyo kwenye hafla fupi iliyofanyika uwanja wa michezo wa Majimaji uliopo mjini hapa, ikishuhudiwa na wananchi ambao walihudhuria hafla hiyo.

Gama alisema kuwa ameamua kununua magari hayo, kupitia mkopo ambao atakuwa anakatwa kwenye mshahara wake kutokana na kuguswa na changamoto zinazowakabili baadhi ya wananchi wake, ikiwemo baadhi yao kutokuwa na uwezo wa kukodi magari ya kuwapeleka hospitali kupata matibabu pale wanapougua ghafla.


"Ndugu zangu nimeamua kununua magari haya ili yaweze kuwasaidia hata kubebea miili ya marehemu waliofariki dunia, hasa pale mnapokumbwa na matatizo ya ukosefu wa usafiri", alisema Gama.

Akizungumza mara baada ya kukabidhi msaada huo, alisema kuwa katika kipindi cha miaka mitano cha uwakilishi wake atahakikisha anajitahidi pia kupunguza kero na changamoto mbalimbali, ambazo zinawakabili wananchi wake ndani ya jimbo la Songea mjini.

Mbunge huyo amewaomba wananchi wa jimbo hilo, kumpa ushirikiano katika utendaji wake wa kazi kwa lengo la kusukuma gurudumu la maendeleo ya jimbo hilo kwa uharaka zaidi.


Kwa upande wao baadhi ya wananchi wa Manispaa ya Songea, kwa nyakati tofauti walimshukuru na kumpongeza Mbunge wao wakieleza kwamba msaada huo utakuwa mkombozi mkubwa kwao hasa akina mama wajawazito, watoto, wazee na vijana.

No comments: