Sunday, July 17, 2016

DED NAMTUMBO AWATAKA WATENDAJI WAKE KUFANYA KAZI KWA VITENDO



Na Yeremias Ngerangera,
Namtumbo.

MKURUGENZI mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Christopher Kilungu amewataka watendaji wa halmashauri hiyo kutekeleza majukumu yao ya kazi, kwa kufuata misingi na taratibu zilizowekwa na serikali.

Aidha wakuu wa idara wametakiwa nao kuacha kuwa na majibu mepesi ambayo hayajitoshelezi katika idara zao, pale watakapohitajika kutoa ufafanuzi kuhusiana na kazi zao za kila siku.

Kilungu alisema hayo juzi alipokuwa kwenye kikao maalumu na watendaji wa halmashauri ya Namtumbo kilichofanyika mjini hapa ambapo aliwataka pia wakuu hao wa idara kufuata sera, kanuni, sheria  na taratibu zilizowekwa kwa kutumia  taaluma  zao.


Vilevile aliwataka kuwa wabunifu na kushauri vitu vyenye manufaa kwa halmashauri hiyo na taifa kwa ujumla, ili kuweza kuleta maendeleo kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Pia aliwataka wakuu hao wa idara kumpa ushirikiano wa dhati katika kusimamia maendeleo ya wananchi, huku akiongeza kuwa yeye amepewa dhamana na serikali katika kuhakikisha kwamba halmashauri ya Namtumbo inasonga mbele kimaendeleo.

“Ndugu zangu tuchape kazi kwa uhakika, tuache majungu na fitina nawataka tufanye kazi kwa vitendo sio maneno”, alisisitiza Kilungu.

No comments: