Saturday, July 30, 2016

URAIA WA NCHI MBILI WAMSHITUA MKUU WA WILAYA NAMTUMBO



Na Yeremias Ngerangera,
Namtumbo.

MKUU wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Luckness Amlima ameshitushwa na taarifa ya uraia wa nchi mbili Msumbiji  na Tanzania ambao unafanywa na wananchi wa kijiji cha Likuyumandela, kata ya Likuyu wilayani humo bila kufuata taratibu husika.

Amlima alishitushwa na taarifa hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani humo, ambayo ilienda sambamba na kuzungumza na wajumbe wa baraza la maendeleo la kata katika kata zote za wilaya ya Namtumbo.

Luckness Amlima katikati, akiwa na kamati yake ya maendeleo.
Akisoma taarifa ya maendeleo kata ya Likuyu kwa Mkuu wa wilaya huyo, Mratibu elimu kata, Ireneus Fusi alisema kuwa pamoja na changamoto zingine kuwepo lakini kata hiyo inachangamoto kubwa kwa wananchi wake, kuwa na makazi ya kuhamahama ambapo wakati mwingine wanaishi Tanzania au Msumbiji.

Fusi alifafanua kuwa hali hiyo ya kuhamahama imekuwa ikiwayumbisha watoto wao hasa kwa wale ambao ni wanafunzi, wanaosoma shule za msingi na sekondari.


Alisema kuwa katika kipindi cha mwaka huu, tayari wanafunzi tisa wa darasa  la saba shule ya msingi Mandela kata ya Likuyu ambao wanatarajia kufanya  mtihani wa taifa darasa la saba, wametorokea nchi ya Msumbiji.

Kufuatia hali hiyo, Ofisa uhamiaji wa wilaya ya Namtumbo Ditrick Kamuhabura alimweleza Mkuu wa wilaya ya Namtumbo, Amlima kuwa ofisi yake ya uhamiaji itapiga kambi katika kata hiyo ili kuweza kujiridhisha kama kweli kuna wananchi wanaishi nchi jirani ya Msumbiji na wakati mwingine Tanzania bila kufuata taratibu husika.

Kamuhabura aliongeza kuwa kijiji cha Likuyumandela, kimetokana na wakimbizi  wa Msumbiji hivyo ofisi yake itafanya mawasiliano na serikali ya nchi hiyo ili kujiridhisha juu ya jambo hilo, kama wananchi hao wanauraia wa nchi mbili au la.

Hata hivyo kwa upande wake Mkuu wa wilaya hiyo, Amlima alisema kuwa endapo kutakuwa na ukweli juu ya tatizo hilo ofisi yake itawataka wananchi hao kuukana uraia wa nchi moja na sio vinginevyo.

No comments: