Thursday, July 7, 2016

JESHI LA POLISI RUVUMA LAMSHIKILIA MTOTO WA MWENYEKITI HALMASHAURI WILAYA YA MBINGA KWA TUHUMA YA UBAKAJI

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma, linamshikilia Justine Ambrose Nchimbi (30) ambaye ni mtoto wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani humo kwa tuhuma ya kumbaka mwanafunzi wa shule ya wasichana ya sekondari Mbinga, iliyopo katika kata ya Kigonsera wilayani humo.

Aidha kwa mujibu wa taarifa zilizomfikia mwandishi wetu na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Zubery Mwombeji zinaeleza kuwa tukio hilo lilitokea Julai 2 mwaka huu majira ya usiku katika kijiji cha Kitai wilayani hapa.

Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania, Ernest Mangu.
Mwombeji alisema kuwa mwanafunzi huyo ambaye ana umri wa miaka 14 anasoma kidato cha kwanza katika shule hiyo na kwamba alibakwa na kijana huyo, ambaye ni mfanyakazi wa kukusanya mapato ya halmashauri ya wilaya hiyo katika geti la Kitai ambapo alitumia nguvu kwa kumvuta mtoto huyo na kumuingiza kwenye kibanda cha walinzi kilichopo katika eneo hilo na kumfanyia unyama huo.

Alisema kuwa mtoto huyo wakati anafanyiwa kitendo hicho alikuwa akitokea nyumbani kwake kijiji cha Ngingama kata ya Lituhi wilaya ya Nyasa, ambapo alipanda basi na kushuka Kitai majira ya saa mbili usiku ili aweze kusubiri magari yanayotokea Songea kwenda Mbinga na hatimaye aripoti katika shule hiyo anayosoma ili aendelee na masomo yake.


Pamoja na mambo mengine, timu ya waandishi wa habari ambayo iliwasili katika hospitali ya wilaya ya Mbinga ambako mtoto huyo amelazwa kwenye wodi maalumu ya wagonjwa wa bima, imeshuhudia hali yake ikiwa mbaya huku akizungumza kwa shida.

Mwanafunzi huyo aliwaeleza waandishi wa habari kuwa baada ya kushuka basi nyakati hizo za usiku, wakati anasubiri basi lingine ili aweze kuelekea katika shule hiyo anayosoma ndipo ghafla alitokea kijana aliyemtaja kwa jina la Justine Ambrose Nchimbi na kumvuta kwa nguvu kwenye kibanda hicho cha walinzi na kumbaka.

“Wakati anatumia nguvu ya kunivuta kuelekea kwenye kile kibanda nilikuwa nikipiga kelele, yeye alikuwa akikazana kuniziba mdomo lakini sikupata msaada wowote mpaka alipofanikisha kitendo chake cha kunifanyia unyama huu”, alisema mtoto huyo.

Alifafanua kuwa baada ya kufanyiwa kitendo hicho alikuwa akivuja damu nyingi jambo ambalo lilimfanya ashindwe kutembea kutokana na maumivu makali aliyokuwa akiyapata na kulazimika kulala kwenye kibanda hicho mpaka ilipofika majira ya asubuhi Julai 3 mwaka huu, ndipo aliomba msaada kwa wasamaria wema ambao walimsafirisha kwa gari mpaka kituo kikuu cha Polisi wilaya ya Mbinga na kwenda kupatiwa matibabu hospitalini hapo.

“Damu ziliendelea kunitoka kwa muda mrefu huku tumbo langu likiwa linauma sana na sasa sehemu zangu za siri zimevimba bado najisikia maumivu makali mama yangu mzazi alipowasili hapa, amenitolea damu chupa mbili ambazo madaktari wameweza kunifanyia matibabu na kunusuru uhai wangu”, alisema mtoto huyo huku akidondosha machozi.


Hata hivyo mganga mkuu wa hospitali ya wilaya ya Mbinga, Elisha Robert alithibitisha juu ya mwanafunzi huyo kubakwa na kwamba alipotakiwa kutolea maelezo ya kina juu ya hali ya mgonjwa huyo, alikataa na kusema kuwa zitatolewa baadaye mara baada ya afya yake kurejea katika hali ya kawaida.

No comments: