Thursday, October 27, 2016

DC MBINGA AWATAKA VIONGOZI KUONGEZA UWAJIBIKAJI KATIKA KAZI

Na Muhidin Amri,          
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye amewataka viongozi wa vijiji na kata wilayani humo kuongeza uwajibikaji kwa wananchi, hatua ambayo itasaidia kupata ushiriki mkubwa wa wananchi katika shughuli za maendeleo.

Cosmas Nshenye, Mkuu wa wilaya ya Mbinga.
Nshenye alisema hayo juzi Ofisini kwake, alipokuwa akizungumza na mwandishi wa gazeti hili na kubainisha kuwa kuna haja sasa kwa watendaji hao wa serikali kuona umuhimu wa kujituma ipasavyo, katika kuwatumikia wananchi ambao bado wanakabiliwa na matatizo mengi ya kimaisha katika maeneo yao.

Pia Mkuu huyo wa wilaya ya Mbinga, amewataka watumishi wote wa umma kutokuwa chanzo cha matatizo na vurugu kwa wananchi kwani huu ni muda wa kufanya shughuli za maendeleo na kujiepusha vitendo viovu  kama vile ulaji wa fedha za maendeleo zinazopelekwa katika vijiji, kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuimarisha huduma za kijamii.


Kadhalika Nshenye aliwataka kuwa wa wazi katika shughuli zao za kila siku za kiutendaji ikiwa ni pamoja na kusoma taarifa za mapato na matumizi, ambayo yamekuwa chanzo cha migogoro kwa baadhi ya watendaji ili waweze kujijengea uaminifu na kukubalika kwa wananchi wanao waongoza.

Alisema kuwa, kumekuwa na malalkamiko mengi ya wananchi dhidi ya viongozi wao pale ambapo wanashindwa kusoma taarifa hizo jambo ambalo linasababisha kuzusha migogoro isiyokuwa na tija, ukizingatia kwamba kipindi hiki cha serikali ya awamu ya tano kimedhamiria kuboresha huduma zake za kijamii ili kuharakisha upatikanaji wa maendeleo hapa nchini.


“Kazi ya mtumishi wa umma ni kuwawezesha wananchi kuwa na mazingira mazuri ambayo yatawafanya kupenda kushiriki katika kazi za kujitolea nguvu zao kwa ajili ya maendeleo, kama vile  zoezi linaloendelea nchini kote la ufyatuaji tofari kwa ajili ya ujenzi wa matundu ya vyoo, vyumba vya madarasa, nyumba za walimu pamoja na zahanati na vituo vya afya kwa kila kijiji na kata”, alisema Nshenye.

No comments: