Friday, October 7, 2016

KTA YAWAJENGEA UWEZO WAANDISHI WA HABARI NA WAKUFUNZI WA VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI

Waandishi wa habari wakikaribishwa katika mafunzo yanayolenga kuwajengea uwezo wa kufikisha habari katika jamii kwa haraka zaidi na kwamba, mafunzo hayo yanasimamiwa na Shirika la Karibu Tanzania Association (KTA).  
Na Kassian Nyandindi,           
Iringa.

WAANDISHI wa habari hapa nchini, wametakiwa kujijengea ujasiri na kuacha kukata tamaa pale wanapokumbwa na vikwazo wakati wanapofanya kazi zao, badala yake wazingatie maadili ya taaluma yao ili jamii iendelee kuwathamini na kuheshimu vyombo vya habari.

Aidha imeelezwa kuwa tasnia ya habari, ndiyo fani mtambuka inayoweza kuwafanya wananchi waweze kusonga mbele kimaendeleo kwa faida ya kizazi cha sasa na hapo baadaye.

Mwenyekiti wa taifa, Shirika la Karibu Tanzania Association (KTA) Aidan Mchawa alisema hayo leo alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tatu ya Wanahabari na Wakufunzi wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDC) hapa nchini, yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Neema Craft uliopo katika Manispaa ya Iringa mkoani hapa.


“Kama tasnia hii ya habari isingelikuwepo hakika dunia ingebakia kuwa madudu, Waandishi wa habari wanamchango mkubwa katika jamii na ndio maana maeneo mengi, tunashuhudia matatizo yanayoibuliwa na hawa wenzetu na serikali imekuwa ikichukua hatua za haraka kwa ajili ya manufaa ya taifa letu”, alisema Mchawa.

Kadhalika alieleza kuwa KTA ni shirika lisilokuwa la serikali ambalo ni mwamvuli wa Vyuo vya maendeleo ya wananchi Tanzania, limekuwa likifanya kazi na vyuo hivyo kwa kushirikiana na serikali kwa lengo la kusimamia na kuvifanya viweze kusonga mbele katika masomo na fani mbalimbali zinazotolewa vyuoni humo.

Awali kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Shirika hilo, Maggid Mjengwa alisema kuwa lengo la kuwakutanisha Waandishi wa habari katika mafunzo hayo ni baada ya kuona ni watu ambao wakiungana na Wakufunzi wa vyuo hivyo, wataweza kuijenga nchi na kuendeleza jamii katika tasnia ya habari.


“Ndugu zangu Waandishi wa habari baada ya mafunzo haya mtakwenda pia kusaidia kutoa elimu katika hivi vyuo vyetu vya maendeleo ya wananchi, malengo yetu ni kuifanya jamii itambue pia umuhimu wa tasnia hii ya habari na mafunzo haya yana umuhimu mkubwa katika vyuo vyetu”, alisema Mjengwa.

No comments: