Monday, October 31, 2016

SERIKALI MBINGA KUENDELEA KUWACHUKULIA HATUA WALANGUZI WA KAHAWA



Na Kassian Nyandindi,              
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye amesema kwamba asilimia 80 ya kahawa inayozalishwa wilayani humo Wakulima wake hawauzi wao wenyewe katika minada ya kuuzia zao hilo, bali imekuwa ikiuzwa na Walanguzi hivyo serikali itaendelea na msako mkali wa kuwakamata watu wanaotumia mbinu hizo za ujanja kuwarubuni wakulima.
Cosmas Nshenye.

Nshenye alisema hayo juzi alipokuwa akitoa salamu za serikali kwenye kikao cha baraza la Madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, ambapo alieleza kuwa katika msimu wa uzalishaji kahawa mwaka huu makampuni kadhaa yalikamatwa na kupigwa faini baada ya kukiuka taratibu na sheria zilizowekwa juu ya manunuzi ya zao hilo.

Aidha alisisitiza juu ya makampuni hayo kuhakikisha kwamba yanalipa malipo ya ya pili ya mkulima na kuachana na biashara haramu ya magoma ambayo humnyonya mkulima na kumfanya aendelee kubaki kuwa maskini.


“Nawataka viongozi wenzangu tuendelee kusimamia hili ili wakulima wetu waweze kulipwa malipo ya pili, sisi tumepewa dhamana na serikali kwa ajili ya kuwatumikia watu”, alisema Nshenye.

Pia aliongeza kuwa sheria ndogo zilizotungwa katika kumsaidia mkulima namna ya kupambana na biashara ya magoma ya kahawa, inatakiwa iendelee kufanya kazi kwa kumsaidia mkulima ili aweze kuwa na kipato kitakachomsaidia kuweza kupata fedha za kununua hata pembejeo za kilimo ambazo ataweza kuendeleza mazao yake shambani.

“Sisi kama halmashauri tumetunga sheria ndogo ambazo sasa tunapaswa kuzisimamia na kumfanya mkulima huyu aweze kunufaika nazo, wewe ukiwa afisa kilimo timiza majukumu yako ya kazi ni aibu kuona kiongozi wa serikali unakuwa wa kwanza kumkandamiza mkulima, atakayebainika atachukuliwa hatua za kisheria”,  alisisitiza.

Hata hivyo akizungumza kwa niaba ya Madiwani wenzake Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Ambrose Mtarazaki alimhakikishia Mkuu wa wilaya hiyo, Nshenye kwamba wataendelea kushirikiana kwa pamoja katika kudhibiti matatizo yanayowakabili wakulima ikiwemo tatizo hili la biashara haramu ya magoma ya kahawa ambalo limekuwa likimtesa mkulima na kumfanya aendelee kubaki kuwa maskini.

No comments: