Wednesday, October 26, 2016

VALENCE: WADAU MBINGA JITOKEZENI KUNUNUA TOFARI ZILIZOCHANGANYWA KWA MCHANGA NA SIMENTI

Vijana wakifanya kazi katika kiwanda cha kuzalisha tofari zilizochanganywa kwa simenti na mchanga ambacho kinaendeshwa na Kampuni ya Ovans Construction Limited, Mbinga mjini mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,            
Mbinga.

HATIMAYE Kampuni ya Ovans Construction Limited iliyopo Mbinga mjini mkoani Ruvuma, imeanza kuzalisha tofari za kuchanganya mchanga na simenti kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za aina mbalimbali, ikiwa ni lengo la kuwataka vijana wanaojishughulisha na kazi ya ufyatuaji tofari za udongo mabondeni katika mji huo waachane na kazi hiyo ambayo inachangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa mazingira.

Aidha uhamasishaji huo wa vijana kuachana na kazi ya ufyatuaji wa tofari za udongo mabondeni ni njia ya kuepukana pia na uharibifu wa vyanzo vya maji ambao unaendelea kushika kasi kila siku katika mji huo.

Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Valence Urio alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa ambapo alifafanua kuwa kazi hiyo ya uundaji wa tofari za udongo pia huchangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa misitu, ambapo wafyatuaji hulazimika kukata miti msituni kwa ajili ya kuweza kupata kuni za kuchomea tofari.


Valence alisema kuwa baada ya kuona uharibifu huo wa mazingira ukiwa unaendelea kushika kasi katika mji huo aliona ni vyema anunue mashine ya kisasa ambayo itaweza kufanya kazi ya kufyatua tofari za kuchanganya mchanga na simenti na kuwataka vijana wanaojishughulisha na kazi hiyo, wajikusanye kwa pamoja na yeye atawasaidia kuunda kikundi ambacho kitasajiliwa kisheria na kuweza kufanya kazi hiyo ya kuwaletea kipato.

“Ninahamasisha vijana wote hapa Mbinga waje kufanya kazi hii, lengo waachane na kazi ya ufyatuaji tofari za udongo kule mabondeni kwani huchangia kuharibu mazingira yetu”, alisema Valence.

Alisema mashine hiyo ambayo ujenzi wake umekamilika na sasa kwa siku inauwezo wa kufyatua tofari za simenti (blocks) 1,600 hivyo anawaomba Wadau na wananchi kwa ujumla kutoka ndani na nje ya Mbinga, kujitokeza kwa wingi kununua tofari hizo ili waweze kukamilishia shughuli zao za ujenzi.

“Tofari tunafyatua kwa wingi kulingana na mahitaji ya mteja, tunafyatua ukubwa wa inchi tano kwa tofari moja shilingi 1,100 na inchi sita kwa shilingi 1,300 na kwamba mteja ambaye anaishi umbali usiozidi kilometa tano kutoka eneo la kiwandani tunapofyatua tofari, tunamsafirishia bure sisi wenyewe mpaka saiti katika eneo lake la ujenzi”, alisema.

Hata hivyo Mkurugenzi huyo wa Kampuni ya Ovans Construction Limited aliongeza kuwa, pia kampuni imeweza kusaidia vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga kuanzisha mradi wa ushonaji nguo na kusimamia mikopo benki ya kikundi cha vijana kinachofahamika kwa jina la ‘Kusile waendesha boda boda’ kilichopo mjini hapa, ili waweze kujipatia kipato na kusukuma mbele gurudumu la maendeleo katika maisha yao.

No comments: