Sunday, October 23, 2016

KAMPUNI YA LEOP AND VIANN MKOMBOZI KWA MKULIMA WA MAHINDI MKOANI RUVUMA


Msimamizi wa ujenzi wa kiwanda cha kusindika nafaka cha Leop and Viann Associates Tanzania Limited, Zeno Komba akitoa maelekezo namna ambavyo mtambo wa kusindika mahindi unavyofanya kazi.

Hapa Zeno Komba akitoa maelekezo juu ya namna ambavyo kipimo cha kielektroniki kinavyofanya kazi wakati wa upimaji mahindi kiwandani hapo.


Na Dustan Ndunguru,

SERIKALI inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli imekuwa ikiendelea na jitihada zake za kuhamasisha Watanzania wazalendo, kujenga dhana ya kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vidogo, vya kati na vikubwa hapa nchini hali ambayo itaifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Ukiachilia mbali Wazalendo, pia inaendelea kuhamasisha wawekezaji kutoka nje ya nchi waweze kuja kuwekeza kwa kujenga viwanda hivyo ambapo katika kufanikisha hilo, serikali inaowajibu wa kuandaa mazingira mazuri ambayo hayatakuwa kikwazo katika kufanikisha zoezi hilo muhimu la uwekezaji.

Watanzania waliowengi wanayo mitaji midogo ambayo kimsingi wanaweza kujikita zaidi katika uanzishaji wa viwanda vidogo nchini kote, ikiwemo maeneo ya vijijini ambako wakulima wamekuwa wakizalisha mazao mbalimbali huku yakishindwa kupata bei nzuri kutokana na kukosa uwezo wa kuyasindika na hivyo kuyaongezea thamani.

Viwanda vidogo ndiyo vyenye uwezo wa kutoa ajira kwa watu wa kada ya chini kwa wingi, ikilinganishwa na viwanda vikubwa ambavyo sehemu kubwa ya kazi zake hufanywa na mitambo hivyo kama mwitikio utakuwa mkubwa itasaidia kuondoa changamoto ya ukosefu wa ajira, tatizo ambalo limekuwa likiwakumba hasa vijana.

Mkoa wa Ruvuma ni moja kati ya mikoa ambayo imebahatika kuwa na ardhi nzuri ambayo wananchi wake wamekuwa wakiitumia kwa kuzalisha mazao mbalimbali ya chakula na biashara, huku changamoto kubwa ikiwa ni kukosekana kwa viwanda vya usindikaji jambo ambalo limekuwa kikwazo kikubwa kwa maendeleo yao.

Kutokana na serikali ya awamu ya tano kuhamasisha wananchi wajitokeze kuanzisha viwanda vidogo na vikubwa, baadhi ya wananchi wameanza kuitikia mwito huo kwa kasi kubwa ambapo wameweza kujitokeza na kuanzisha viwanda vidogo vya kusindika nafaka mkoani hapa na hivyo kupelekea wakulima wapate unafuu kwa njia moja au nyingine, ikiwemo urahisi wa kuuza mazao yao.

Hivi karibuni Mwandishi wetu wa makala haya alipata fursa ya kutembelea katika mtaa wa Namiholo ambao unajumuisha vitongoji vya Mtakuja, Kambarage, Soweto, Kisiwani, Miembeni na Mshikamano kijiji cha Peramiho A kata ya Peramiho, wilayani Songea ambako Kampuni ya Leop and Viann Associates Tanzania Limited imewekeza kwa kujenga kiwanda kidogo cha kusindika nafaka aina ya mahindi, jambo ambalo ni faraja kwa wakulima wa maeneo hayo jirani na mkoa wa Ruvuma kwa ujumla.


Mwenyekiti wa kijiji hicho David Kapinga anasema kwamba, kuanzishwa kwa kiwanda hicho kutasaidia kuinua uchumi wa wananchi wa Peramiho A, kutokana na kuwawezesha kuuza mazao yao karibu ambapo kitendo cha mwekezaji huyo kuanza kununua mahindi kwa ajili ya kiwanda hicho, pia ni mkombozi mkubwa kwa wakulima wake.

Kapinga anasema kuwa serikali kupitia Wakala wa Hifadhi ya Chakula Taifa (NFRA) Kanda ya Songea mkoani hapa mwaka huu imenunua tani 750 kidogo za mahindi kwa kata tatu za Peramiho A, Maposeni na Parango hivyo kupelekea wakulima waliowengi kubaki na mahindi yao majumbani.

“Kwa niaba ya wananchi wangu ninamshukuru mwekezaji huyu kwa kitendo chake cha kununua mahindi kutoka kwa wakulima tena kwa bei ya shilingi 460 ni msaada mkubwa kwetu, kwani walanguzi wamekuwa wakipita vijijini kununua kwa bei ndogo ya shilingi 300 hadi 350”, anasema Kapinga.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Leop and Viann Associates Tanzania Limited, Viann Komba ambaye amejenga kiwanda cha kusindika nafaka za mahindi katika kijiji cha Peramiho A wilaya ya Songea vijijini, mkoa wa Ruvuma na kuwafanya wakulima wanaozalisha zao hilo kupata unafuu wa kuuza jirani mahindi yao kwa bei nzuri.
Anaishauri serikali kuwa na mkakati kabambe wa kuhamasisha wale wenye uwezo kufikiria kuanzisha viwanda katika maeneo ya vijijini ambako nako kuna fursa nyingi za kiuchumi, ifanye hivyo ili kuweza kusaidia kuwainua wakulima ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakitumia nguvu nyingi kuzalisha mazao mbalimbali huku wakishindwa kunufaika nayo kutokana na kukosa kwa kwenda kuyauza.

Mkulima Joseph Nyoni anapongeza kitendo cha mwekezaji wa kiwanda hicho kidogo cha kusindika nafaka kununua mahindi yao kwa kutumia kipimo cha elektroniki, ikilinganishwa na wanunuzi waliowengi ambao wamekuwa wakitumia vipimo ambavyo hulenga kumwibia mkulima kwani huvichezea kila wakati tofauti na hicho cha kisasa ambacho ni vigumu kumwibia mkulima.


Nyoni anabainisha kuwa serikali inaowajibu mkubwa wa kuhakikisha kwamba kipimo kama hicho ambacho hutumiwa na mwekezaji wa kiwanda hicho cha Leop and Viann Asosociates Tanzania Limited, kinatumiwa pia na wanunuzi wengine ili kumnufaisha mkulima ambaye kimsingi ndiye mvuja jasho.

Wakulima Consolata Mwanja, Flora Ndimbo na Adelphina Haulle wanafafanua kuwa kitendo cha serikali kuhamasisha wawekezaji kuwekeza kwa kuanzisha viwanda vidogo vidogo ikiwemo vya kusindika nafaka kumetoa fursa kwa wakulima hasa wadogo, kunufaika kutokana na urahisi wa kuuza mazao yao kwa bei nzuri ikilinganishwa na hapo awali ambapo wafanyabiashara walanguzi walikuwa wakipita kuwarubuni majumbani kwao wawauzie kwa bei ya chini huku wao wenyewe wakinufaika kwa kuuza kwa bei ya juu.

“Mwaka huu tutaongeza uzalishaji wa zao hili la mahindi kutokana na kuwa na uhakika wa soko la kuuzia ambalo lipo hapa hapa kijijini kwetu, ikilinganishwa na hapo awali wanunuzi tulikuwa tukitegemea watoke mijini”, wanasema.

Severine Haulle anaeleza kuwa uwepo wa kiwanda hicho cha kusindika nafaka za mahindi katika kata ya Peramiho, kumesaidia pia kuhamasisha wakulima wakipende kilimo cha zao hilo ambapo sasa kuanzia msimu ujao wa kilimo wengi wao watazalisha kwa wingi zao hilo la chakula na biashara na kwamba anamwomba mwekezaji wa kiwanda hicho kuanza kununua mapema msimu ujao ili wakulima waweze kunufaika na bei nzuri wanayonunua.

Haulle anaeleza kuwa wamechoka kuibiwa mazao yao na wanunuzi ambao kwa miaka mingi wamekuwa kikwazo kwao katika kukabiliana na umaskini wa kipato hivyo kitendo cha kiwanda hicho kujengwa karibu nao kutasaidia wajikwamue kiuchumi ikilinganishwa na hapo awali.

Diwani wa kata ya Peramiho, Issack Mwimba anasema kuwa kiwanda hicho kidogo cha kusindika nafaka kimekuja wakati muafaka ambapo jukumu la viongozi ni kuhakikisha wanahamasisha wananchi, wajikite zaidi katika uzalishaji wa mazao hayo kwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu ili wapate mazao yenye ubora unaohitajika.

Mwimba anafafanua kuwa anauhakika kwamba, uwepo wa kiwanda hicho chenye dhamira ya kusindika mahindi katika kata yake kitaweza kubadilisha maisha ya wananchi anaowaongoza, hususan wale ambao watajikita na uzalishaji wa zao hilo la mahindi na kwamba anamtaka mwekezaji huyo msimu ujao ajitahidi kufungua soko la ununuzi wa mahindi mapema ili kuweza kuwakomesha wanunuzi wenye tabia ya kuwaibia wakulima.

Anasema kiwanda hicho kitasaidia kutoa ajira kwa wananchi wake hivyo anamtaka mwekezaji kuwapa kipaumbele wananchi wa kata hiyo na kwamba vijana wanapaswa kujiunga na vyuo vya ufundi vya VETA, ili waweze kupata ujuzi ambao utawawezesha kupata ajira katika viwanda vinavyoanzishwa kwenye maeneo yao kwani bila kufanya hivyo watashuhudia wakipata ajira watu wa mbali na kuzua malalamiko yasiyo na maana.

“Ni wazi kuwa uanzishwaji wa kiwanda hiki utapunguza changamoto ya ukosefu wa ajira hasa kwa vijana na hivyo kukuza uchumi, sio tu kwa wananchi wa kata hii na jirani bali pia hata kwa taifa letu kwa ujumla”, anasema Mwimba.

Diwani huyo pia anasisitiza juu ya wakulima kuacha tabia ya kuuza mazao yote bila kujiwekea akiba ya kutosha ya chakula na kwamba anawaasa wataalamu wa kilimo katika kata hiyo ya Peramiho, kuhakikisha wanapita kwa wakulima kutoa elimu ya namna bora ya uandaaji wa mashamba kwa ajili ya msimu ujao wa kilimo ili waweze kuzalisha mazao mengi zaidi na yenye ubora kwani msimu wa kilimo umekaribia kuanza.

Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Peramiho, Jenista Mhagama anasema serikali inadhamini sekta binafsi hivyo kuanzishwa kwa kiwanda hicho inaonesha jinsi gani Watanzania wazalendo, wanavyounga mkono juhudi za Rais Dkt. John Magufuli za kuhakikisha kwamba nchi inakuwa ya viwanda na hivyo kusaidia kukuza uchumi wa taifa.

Jenista ambaye pia ni Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu anapongeza kazi ambayo imeonyeshwa na mwekezaji wa kiwanda hicho jimboni kwake.

“Kwa niaba ya serikali nishukuru wale waliowaza kuanzisha kiwanda hiki hapa, kwa kweli kitakuwa msaada mkubwa kwa wananchi wangu wa Peramiho lakini pia niwaombe watu wengine kujitokeza kuwekeza ndani ya mkoa wa Ruvuma na maeneo mengine ya nchi hii, ili dhamira ya serikali ya awamu ya tano ya kuifanya nchi kuwa ya viwanda iweze kutimia kwa manufaa ya wananchi wote”, anasema.

Anawaasa wananchi wanaoishi karibu na kiwanda hicho kujenga ushirikiano mzuri na mwekezaji huyo ili kuondokana na migogoro ambayo mara nyingi imekuwa ikijitokeza pindi mtu anapowekeza na kwamba alilitaka Shirika la Umeme nchini (TANESCO) kuhakikisha linaharakisha kupeleka umeme katika eneo hilo la kiwanda ili kiweze kuanza kazi kwa wakati na hivyo kunufaisha wananchi hususani wale ambao watapata ajira.

Mkurugenzi wa kiwanda hicho, Viann Komba anasema lengo hasa la uanzishwaji wake ni kuunga mkono jitihada za serikali ya awamu ya tano ambayo imedhamiria kuifanya Tanzania kuwa ya viwanda vikiwemo vidogo na kwamba waliamua kuanzisha katika eneo hilo la kijijini ili kuongeza fursa kwa wananchi wa vijiji vinne vya Lundusi, Peramiho A, Peramiho B na Nguvu moja kuwaondolea changamoto ya kukosa masoko ya mazao wanayozalisha.

Komba anafafanua kuwa anauhakika mradi huo kwa kiasi kikubwa utasaidia kuinua uchumi wa wananchi ambapo kiwanda hicho kinao uwezo wa kukoboa na kusaga magunia 200 ya mahindi kwa siku.

Anaeleza kuwa kiwanda hicho cha kusindika nafaka za mahindi kitakuwa na uwezo wa kuajiri wafanyakazi 30 wa kudumu na kwamba wafanyakazi wa muda ambao watakuwa wakifanya kazi kila siku watakuwa 70 na hivyo kufanya kuwa na jumla ya wafanyakazi 100.

Akizungumzia kuhusu kipimo kinachotumika kupimia mahindi yanayoletwa na wakulima kiwandani hapo kwa ajili ya kuuza anasema wameamua kutumia kipimo cha kielektroniki kutokana na ukweli kwamba, kinawatendea haki wakulima ikilinganishwa na vipimo vingine ambavyo ni rahisi kuvichezea ili kumpunja mkulima.

“Sisi hatujaanzisha kiwanda hiki kwa lengo la kumwibia mkulima bali kujenga urafiki naye kwa kununua mazao anayozalisha kwa bei nzuri, ili naye hatimaye aweze kujikwamua kiuchumi na sio vinginevyo lakini pia niwaombe wananchi wanaozunguka kiwanda hiki, wazalishe mahindi yenye ubora ili wanufaike na bei kubwa”, anasisitiza.

Komba anaeleza kuwa dhamira ya serikali ya kuhamasisha wananchi wazalendo wajitokeze kuanzisha viwanda vidogo ikiwemo maeneo ya vijijini ni kutaka mkulima anufaike kwanza kwa kuuza mazao yake kwa urahisi na bei nzuri lakini pia kuongeza thamani ya mazao hayo kwa njia ya usindikaji.

Pamoja na mambo mengine changamoto kubwa inayowakabili katika eneo palipojengwa kiwanda hicho, ni kutokuwepo kwa umeme wa uhakika hivyo Shirika la Umeme nchini (TANESCO) mkoani Ruvuma linaombwa kuharakisha zoezi la upelekaji wa nishati hiyo, ili kiweze kuanza kazi mara moja kama ilivyokusudiwa.

Kuanzishwa kwa kiwanda cha kusindika nafaka cha Leop and Viann Associates Tanzania Limited chenye uwezo wa kusaga tani 15 kwa siku, kutasaidia kupunguza changamoto ya soko la mahindi lililopo mkoani Ruvuma ambapo katika kipindi cha mwaka huu, ulikadiria kuzalisha tani 840,000 za mahindi ambapo Wakala wa Hifadhi ya Chakula ya Taifa (NFRA) Kanda ya Songea katika kipindi hicho amenunua tani 22,000 na kwamba kati ya hizo tani 840,000 nusu yake zimebaki majumbani kwa wakulima kwa ajili ya chakula.

Serikali kwa nchi nzima imekadiria kununua tani laki moja za mahindi pekee, hivyo ni wazi kuwa wakulima watabaki na mahindi mengi majumbani kwao na kulazimika kutafuta soko maeneo mengine, ambako huko ndiko watakakokutana na wanunuzi walanguzi ambao hununua kwa bei ya chini.

No comments: