Wednesday, October 5, 2016

MANISPAA YA SONGEA KUWALETEA NEEMA WANANCHI WAKE KUPITIA MIRADI INAYOSIMAMIWA KWA USHIRIKIANO NA BENKI YA DUNIA

Na Kassian Nyandindi,        
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma imepanga kutekeleza miradi nane iliyopo chini ya mradi wa uendelezaji miji na manispaa, katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2017/2018 kwa lengo la kuwaletea maendeleo wananchi wake kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye. 

Hii ni moja kati ya sehemu ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisa habari wa Manispaa hiyo, Albano Midelo alisema kuwa Manispaa hiyo ni miongoni mwa halmashauri 18 hapa nchini ambazo zinatekeleza mradi huo ambao unasimamiwa na serikali ya Tanzania kwa ushirikiano na benki ya dunia.

Midelo alisema kuwa Manispaa ya Songea, inatarajia kutumia zaidi ya shilingi bilioni 21.8 katika kutekeleza miradi ya uendelezaji miji yake na manispaa hiyo ambayo itatekelezwa katika kipindi cha miaka mitatu.


Vilevile Raphael Kimary ambaye ni mchumi Mkuu wa Manispaa ya Songea, aliitaja miradi hiyo kuwa ni ya ukarabati wa barabara kwa kiwango cha lami kilometa 15 ambayo itagharimu shilingi milioni 11.5 na ununuzi wa magari ya kuzolea taka, yatakayogharimu shilingi bilioni 1.14.

Miradi mingine ni ujenzi wa stendi mpya ya magari ya abiria (mabasi) katika eneo la shule ya Tanga mjini hapa, kwa gharama ya shilingi bilioni 5 na ujenzi wa machinjio ya kisasa itakayogharimu shilingi bilioni 2.1.

Vilevile katika utekelezaji huo kutakuwa na ukarabati wa dampo la kuchomea taka kwa gharama ya shilingi bilioni1.5, kujenga uwezo watumishi na viongozi wa kisiasa kwa gharama ya shilingi milioni 200 na ukarabati wa bustani ya manispaa hiyo kwa shilingi milioni 300.

Kimary amezitaja changamoto zinazosababisha miradi kushindwa kutekelezwa kwa wakati ni kutokana na kutopatikana kwa fedha za miradi kwa muda uliopangwa, kuchelewa kupata kibali cha athari za mazingira katika maeneo ambayo miradi inatekelezwa toka Baraza la Mazingira la Taifa (NEMC) jambo ambalo linasababisha kuchelewa kuanza kazi husika.


Baraza la madiwani wa halmashauri ya Manispaa ya Songea wameunga mkono juu ya taarifa ya utekelezaji wa program hiyo ya uendelezaji wa manispaa hiyo na kushauri pia mradi wa bustani ya manispaa hiyo, ufanyiwe ukarabati mapema kwani nao imekuwa ni chanzo cha mapato kutokana na wakazi wengi wa Songea kununua miche ya miti inayozalishwa hapo na kwenda kuipanda katika maeneo yao kwa lengo la kutunza mazingira.

No comments: