Monday, September 14, 2015

BODI YA KAHAWA YASIKITISHWA WAKULIMA KUTOZINGATIA KANUNI ZA UBORA WA KAHAWA

Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

BODI ya Kahawa Kanda ya Ruvuma ambayo makao makuu ya ofisi yake ipo wilayani Mbinga mkoani humo, imesikitishwa na vitendo vya baadhi ya wakulima wa zao hilo wilayani hapa, kwa kutozingatia kanuni za ubora wa kahawa, jambo ambalo linachangia kushuka kwa uzalishaji wa zao hilo.

Aidha imekemea na kuwataka wakulima hao, kuacha tabia ya kuanika kahawa chini jambo ambalo nalo huchangia kushuka kwa ubora wake, badala yake wanatakiwa kuanika kwenye vichanja vyenye urefu wa mita moja kutoka ardhini, ili isiweze kupata vumbi na thamani yake isiweze kuporomoka.

Peter Bubelwa ambaye ni Meneja wa kanda hiyo, alisema hayo wakati alipokuwa akijibu maswali ya mwandishi wetu ambaye alitembelea ofisini kwake, kutaka kujua maendeleo ya uzalishaji wa zao la kahawa ya wilaya ya Mbinga ambapo ni wilaya pekee mkoani Ruvuma, inayozalisha zao hilo kwa wingi.


Bubelwa alisema kuwa hali ya ubora kimsingi hairidhishi huku akiwataka wakulima wazingatie taratibu za uvunaji, kutayarisha kahawa kwa wakati ikiwemo kutumia mitambo ya kisasa, hasa pale wanapokoboa kahawa mbivu mara baada ya kuivuna shambani.

Pia alieleza kuwa wadau wengi huko vijijini wilayani humo, wamekuwa wakisema hali ya udhibiti wa ubora kwa zao hilo imekuwa sio nzuri huku akiitaka kamati ya ulinzi ndani ya wilaya hiyo ambayo imepewa jukumu la kusimamia hilo kutekeleza majukumu yake ipasavyo, ili kuweza kunusuru hali hiyo isiweze kuendelea kuwepo katika maeneo mbalimbali.

Alisema kuwa serikali imewekeza mitambo (CPU) ya kukoboa kahawa ambayo mkulima analazimika kuitumia ili kahawa iweze kuwa na ubora, ambapo kwa wilaya ya Mbinga kuna mitambo 155 ambayo inafanya kazi.

“Jumla ya tani 13,000 za kahawa kavu, kwa msimu huu tunakadiria kuzivuna hapa wilayani lakini mpaka kufikia Agosti 31 mwaka huu, tayari tani 5,490 za kahawa kavu zimekusanywa kutoka kwa mkulima shambani tayari kwa kupelekwa kiwandani kukobolewa”, alisema Bubelwa.


Hata hivyo aliwataka wakulima waachane na tabia ya kuchakata kahawa majumbani, kwani ubora wake umekuwa ukipungua na kuifanya ikose soko na bei nzuri pale inapouzwa mnadani Moshi.

No comments: