Sunday, September 13, 2015

TUNDURU WATAKIWA KUTOGAWA ARDHI YAO KWA WAGENI

Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

WANANCHI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wameaswa kujiepusha na vishawishi vinavyosababisha kuuza ardhi yao kwa wageni bila kufuata taratibu za nchi, ikiwa ni lengo la kuwafanya waweze kuepukana na vitendo vya uporaji vinavyofanywa na watu wajanja, hatimaye kuwa maskini na watumwa katika nchi yao.

Badala yake wametakiwa kutumia utajiri wa ardhi waliyonayo, kuzalisha kwa wingi mazao mbalimbali ili wajikwamue na waondokane na umaskini.

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mohamed Lawa alisema hayo alipokuwa akizungumza na wanachama wa chama hicho, katika kijiji cha Nandembo kwenye ziara yake ya kikazi ya kuhamasisha wananchi kushiriki katika mikutano ya kampeni ya wagombea wa chama hicho, inayoendelea sasa hapa nchini.


Lawa alisema kuwa mipaka ya Tunduru na maeneo mengine ya nchi, imeanza kufunguka hivyo anaimani wilaya itapokea wageni wengi kutoka ndani na nje ya nchi, ambao watahitaji maeneo kwa ajili ya shughuli za kiuchumi hivyo wanaowajibu wa kutunza ardhi yao kwa faida ya vizazi vya sasa na baadaye.

Alisema kuingia kwa wageni hao ni jambo zuri ambalo litasaidia kukua kwa uchumi wa wilaya hiyo, lakini itakuwa sio jambo la busara kuona wananchi wanauza maeneo yao kiholela bila kufuata taratibu na ushauri kutoka kwa wataalamu husika, na kubaki mwisho wa siku wanahangaika kutokana na kuuza kwa bei ndogo ambayo hailingani na thamani halisi.

“Nawataka wananchi watumie ardhi yao kwa shughuli za maendeleo yao na sio kukimbilia kuwauzia wageni, wakati sisi wenyewe tukiendelea kubaki maskini”, alisema Lawa.

Kadhalika aliipongeza serikali ya chama tawala kwa utekelezaji wa ahadi zake kwa wananchi wa wilaya ya Tunduru, kwani kumekuwa na dalili tosha za kuvutia wageni kwenda kuwekeza huko ambapo wilaya hiyo ni kati ya wilaya chache ambazo zimebahatika kuzungukwa na madini ya aina mbalimbali, misitu, ardhi na wanyama.


Mbali na hilo alisema kujengwa kwa barabara ya lami kutoka Namtumbo, kwenda Tunduru hadi Masasi na kuanza utekelezaji wa mradi wa umeme vijijini (REA) ni ishara kubwa kwamba serikali imedhamiria kumaliza kero zilizokuwa zinakwamisha maendeleo ya wananchi wake.

No comments: