Friday, September 4, 2015

GAMA: EPUKENI KUCHAGUA VIONGOZI WATOA RUSHWA

Leonidas Gama.
Na Muhidin Amri,
Songea.

WAKATI kampeni zikiendelea kwa wagombea wa vyama mbalimbali vya siasa, nafasi ya Rais, mbunge na diwani wito umetolewa kwa wananchi wa Jimbo la Songea mkoani Ruvuma kuepuka kuchagua viongozi watoa rushwa, kwani kufanya hivyo hakutaweza kusaidia kupata kiongozi bora atakayeweza kuwaongoza wananchi.

Mwito huo umetolewa na mgombea ubunge wa jimbo hilo, Leonidas Gama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu mjini hapa.

Gama ambaye pia ni Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, amewataka wanaccm kuungana pamoja ili kuweza kuleta ushindi wa kishindo katika uchaguzi ujao na sio kuendeleza majungu na makundi ndani ya chama hicho, ambayo yanahatarisha uvunjifu wa amani katika jamii hasa kipindi hiki kuelekea uchaguzi mkuu.

“Nawaomba wanachama wenzangu wa Chama Cha Mapinduzi, tuvunje makundi tuungane pamoja ili tuwashinde wagombea wa vyama vingine vya siasa”, alisema Gama.


Alifafanua kuwa wananchi wanapaswa kutumia haki yao ya kidemokrasia, kuwasikiliza wagombea wote wa vyama hivyo ili waweze kuwapima na baadaye kufanya maamuzi sahihi, yatakayoleta ufanisi katika kumchagua kiongozi bora na sio bora kiongozi.

Gama alieleza kuwa ni vyema wananchi wakatambua kwamba, kumchagua kiongozi anayetoa rushwa sio njia ya kukuza demokrasia ya kweli hivyo utoaji rushwa, madhara yake ni kuwapata viongozi wabovu na wenye uchu na madaraka ambao hawana dhamira ya kweli, katika kuwasaidia wananchi kusukuma mbele maendeleo yao.


Alisema kiongozi anayepatikana kwa mtindo huo, jambo la kwanza hushibisha tumbo lake kipindi aingiapo madarakani kwa kuhakikisha anarudisha fedha zake alizowahonga wapiga kura wakati wa kampeni, huku akiwaacha wananchi wakiendelea kuteseka na kero zinazowakabili katika maeneo yao.

No comments: