Saturday, September 12, 2015

NYASA WAIPONGEZA NMB KWA KUANZISHA HUDUMA ZA KIFEDHA

Ziwa Nyasa lililopo wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,
Nyasa.

BAADHI ya wananchi wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, wamepongeza jitihada zinazofanywa na Benki ya NMB kwa kuanzisha na kutoa huduma za kifedha wilayani humo, jambo ambalo limekuwa ni mkombozi kwao katika kuendeleza biashara zao.

Walisema kitendo cha benki hiyo kutoa huduma ya kufungua akaunti, kulipa hundi, kuweka na kutoa fedha kwa kutumia mfumo wa Benki jamii (Bank on Wheel) kumeweza kuwapunguzia umbali mrefu wa kufuata huduma hiyo ambapo awali walikuwa wakilazimika kwenda wilaya ya Mbinga, ili waweze kupata mahitaji ya kifedha katika taasisi hiyo ya kifedha.

Aidha walifafanua kuwa wilaya ya Nyasa ni wilaya mpya, ambayo tokea kuanzishwa kwake sasa ni faraja kwa wananchi wa wilaya hiyo, kusogezewa karibu huduma hiyo muhimu kwa faida ya maendeleo yao.


Hayo yalisemwa na wananchi wa wilaya hiyo, walipokuwa wakizungumza na mwandishi wetu na kuongeza kuwa kutokana na wilaya kuwa na watu wanaojishughulisha na shughuli mbalimbali, kama vile uvuvi wa samaki na wakulima wa zao la kahawa sasa wataweza kufanya biashara zao kwa ufanisi zaidi kutokana na kusogezewa karibu huduma za kifedha.

“Tunawapongeza watu hawa wa NMB kwa kuwa na wazo la kuanzisha huduma hii muhimu hapa kwetu, hata uchumi wa wilaya yetu ya Nyasa utaweza kukua na kusonga mbele kimaendeleo”, alisema Aden Komba.

Komba ambaye ni mkazi wa kijiji cha Kilosa kata ya kilosa wilayani humo, alibainisha kuwa jitihada hizo zinazofanywa na benki  hiyo ili ziweze kuleta mafanikio, kuna kila sababu NMB ikafanya mpango wa kujenga ofisi za kudumu za kutolea huduma za kifedha katika wilaya hiyo, ili wananchi waweze kupata hata huduma za mikopo kwa karibu zaidi.


Vilevile kwa upande wa wafanyakazi ambao wameajiriwa na serikali kwenda kufanya kazi katika wilaya hiyo ya Nyasa, nao walipongeza jitihada hizo na kueleza kuwa kila mwishoni mwa mwezi walikuwa wakilazimika kufuata huduma za mishahara wilayani Mbinga, ambako ni mbali kutoka wilayani humo lakini sasa imekuwa kwao ni rahisi kupata huduma hiyo.

No comments: