Monday, September 7, 2015

TASAF NAMTUMBO YAJIVUNIA MAFANIKIO YAKE KAYA MASKINI ZANUFAIKA NA MPANGO WAKE

Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

SERIKALI imelipa kiasi cha shilingi milioni 257,004,000 kwa kaya maskini 56 ambazo ziliibuliwa wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, kupitia mpango wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) awamu ya tatu ili ziweze kuwasaidia kugharimia mahitaji yao muhimu, ikiwemo matibabu, chakula na kulipa karo za watoto wao shuleni.

Ofisa ushauri na ufuatiliaji kutoka katika mfuko huo wilayani humo, Edson Kagaruki alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, huku akiwataka walengwa walioibuliwa kwenye mpango huo kutumia fedha hizo kwa malengo yaliyokusudiwa na sio kunywea pombe au kuongeza idadi ya wake majumbani kwao.

Kagaruki alisema, baada ya zoezi la uandikishaji na usajili waliweza kuibua kaya hizo kutoka katika vijiji 42, ambavyo viliingizwa kwenye mpango huo wa awamu ya tatu.


Alisema kuwa serikali kupitia mpango wa TASAF, imekuwa ikitoa ruzuku ya msingi na ile ya masharti nafuu kwa kaya hizo na familia zinazoishi katika mazingira hatarishi, ili ziweze kumudu kupata mahitaji yao ya kila siku na kwamba mpango huo ni wa miaka mitatu ambapo kila kaya, italipwa fedha kwa miezi miwili miwili.

Ruzuku ya msingi imekuwa ikitolewa kwa kila kaya, ambayo imeandikishwa kwenye mpango huo na ile yenye masharti nafuu hutolewa kwa kaya maskini ambazo zina watoto wanaohitajika kwenda shule na wale wanaohitaji kupata huduma ya matibabu, ambao wana umri chini ya miaka mitano.

Kadhalika kwa kila kaya au familia kupitia mpango huo, huweza kuboresha maisha yao kwa kuweka akiba, uanzishwaji wa shughuli ndogo ndogo za kiuchumi ambapo kwa kipindi hicho cha miaka miwili hupatiwa ruzuku ya shilingi 36,000 hadi 65,000 ambazo hutolewa kila baada ya miezi miwili.


Hata hivyo aliongeza kuwa kazi ya uzinduzi wa malipo kwa kaya hizo ulitekelezwa rasmi Agosti 18 mwaka huu, katika kijiji cha Namtumbo na Mkuu wa wilaya hiyo Chande Nalicho.

No comments: