Saturday, August 19, 2017

BARAZA LA MADIWANI MBINGA LAMALIZA MVUTANO UJENZI WA MAKAO MAKUU OFISI ZA HALMASHAURI YA WILAYA

Madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga wakiwa katika kikao chao cha baraza la madiwani.
Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga Gombo Samandito aliyesimama amevaa joho rangi nyekundu, akisimamia zoezi la kuhesabu kura ni wapi Madiwani wa wilaya hiyo wamechagua sehemu ambayo kutajengwa Ofisi za makao makuu ya halmashauri hiyo.
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

BARAZA la Madiwani katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma limepitisha kwa pamoja na kukubaliana kwamba, ujenzi wa Ofisi za makao makuu ya wilaya hiyo zitajengwa katika eneo maarufu linalofahamika kwa jina la Ndengu lililopo katika kata Nyoni wilayani humo.

Maamuzi hayo yalifikiwa juzi katika kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa, baada ya uwepo wa mvutano mkubwa uliodumu kwa masaa kadhaa kati ya Madiwani hao na Watendaji wa halmashauri hiyo juu ya wapi Ofisi hizo zitajengwa.

Awali zilipopigwa kura kwa lengo la kukubaliana kwamba ujenzi huo ukafanyike katika eneo la Kiamili lililopo katika kata ya Kigonsera, Madiwani hao walikataa na kukubaliana kwamba zipigwe kura kwa mara ya pili kwa kuchagua kati ya eneo la Maguu, Ndengu na Matiri.


Zilipopigwa kura kuchagua katika maeneo hayo ndipo waliweza kuchagua eneo hilo la Ndengu ambalo lilishinda kwa kura 24, likifuatiwa na Matiri kwa kura 9 na Maguu kwa kura 1 huku kura mbili zikiharibika kati ya wapiga kura 36 waliokuwepo katika kikao hicho.

Matokeo hayo ya makubaliano wapi ukafanyike ujenzi wa Ofisi hizo za makao makuu ya halmashauri ya wilaya ya Mbinga juu ya eneo hilo lililoshinda kwa kura nyingi yalitangazwa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Gombo Samandito mbele ya kikao cha baraza hilo mara baada ya uchaguzi huo kufanyika.

“Mheshimiwa Mwenyekiti kura za Ndengu ni 24 kwa hiyo napenda kutangaza kwamba kwa mujibu wa kura hizi halali eneo la halmashauri kuu ya wilaya yetu litakuwa ni Ndengu”, alisema Samandito.

Naye Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Ambrose Nchimbi aliongeza kuwa yeye anaamini kwamba miundombinu ya majengo ya halmashauri hiyo itakapojengwa hapo itakaa vizuri na kwamba watakachokifanya ni kuongea na Wizara husika ili iweze kutangaza eneo hilo kwamba sasa linafaa kwa kujengwa makao makuu ya wilaya hiyo.

“Kura ambazo Ndengu tumezitoa ninahakika kabisa sasa ugomvi umekwisha tubaki Madiwani kuwa wamoja juu ya kukamilisha zoezi hili la ujenzi wa miundombinu hii ya halmashauri yetu”, alisisitiza Nchimbi.


Pamoja na mambo mengine, kwa ujumla halmashauri hiyo imefikia hatua ya kuhama katika Ofisi zake za awali zilizopo mjini hapa na kwenda kujenga miundombinu mingine mipya ya wilaya hiyo, baada ya kugawika na kuizaa halmashauri nyingine ya mji wa Mbinga ambayo ndiyo inapaswa kutumia majengo hayo yaliyopo sasa mjini hapa.

No comments: