Monday, August 28, 2017

WAKURUGENZI RUVUMA WAPIGWA MARUFUKU KUBADILI MATUMIZI YA FEDHA

Kutoka upande wa kulia ni Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dokta Binilith Mahenge, katikati ni Katibu tawala wa mkoa huo Hassan Bendeyeko na upande wa kushoto ni Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mkoani humo Suleiman Mwaliwale.
Na Kassian Nyandindi,    
Songea.

DOKTA Binilith Mahenge ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma amepiga marufuku Wakurugenzi wa halmashauri za wilaya mkoani humo, kubadilisha matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo ya wananchi bila kuwa na kibali maalum.

“Lazima tufuate kanuni na sheria zilizowekwa, huwezi kubadilisha matumizi ya fedha kutoka sehemu fulani kwenda kwenye mradi fulani wa maendeleo bila kibali maalum, cha msingi hapa ni lazima tufuate taratibu na sheria zilizowekwa”, alisisitiza.

Alitoa onyo hilo juzi alipokuwa akifunga kikao cha utekelezaji wa hoja na mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mkoani humo kwa mwaka 2015/2016 kilichofanyika juzi kwenye ukumbi wa Ikulu ndogo uliopo Songea mjini.


Dokta Mahenge alisema ni aibu na kosa kubwa kwa halmashauri kuwa na hoja za muda mrefu za CAG ambazo hazijibiwi kwa wakati na kwamba alisisitiza watendaji ndani ya halmashauri zao kuona umuhimu na kuipatia uzito taarifa ya Mkaguzi huyo wa hesabu za serikali kwa kutekeleza maagizo yake kwa wakati.

Vilevile alisema kuwa makundi ya vijana, walemavu, wanawake na wazee yatengewe fedha kupitia vikundi vyao vya miradi ya maendeleo ambavyo wamejiunga ili waweze kuondokana na umaskini.

Kadhalika alieleza pia Wakurugenzi hao wanapaswa kutenga maeneo ya ujenzi wa viwanda katika halmashauri zao ambapo viongozi wote waliopo katika eneo husika amewataka pia washirikiane katika utekelezaji wa jambo hilo ili kuweza kuleta ufanisi mzuri.


No comments: