Tuesday, August 29, 2017

BILIONI 14 KUJENGA BARABARA ZA LAMI MANISPAA YA SONGEA

Wataalamu wa Manispaa ya Songea wakikagua moja kati ya barabara ambazo zimejengwa kwa kiwango cha lami kwa ufadhili wa Benki ya dunia.
Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

MANISPAA ya Songea mkoani Ruvuma inatarajia kutumia zaidi ya shilingi bilioni 14.320 katika ujenzi wa barabara zake za mji huo kwa kiwango cha lami zenye urefu wa kilometa 8.6.

Afisa habari wa Manispaa hiyo, Albano Midelo alisema kuwa fedha za mradi huo zimetolewa na Benki ya dunia chini ya Mpango wa kuzijengea uwezo serikali za mitaa (ULGSP) kwa lengo la kuendeleza miundombinu ya halmashauri za Miji na Manispaa 18 zilizopo Tanzania bara ikiwemo Manispaa hiyo ya Songea.

Mradi huo ambao ulianza Juni Mosi mwaka 2015 alieleza kuwa ulitarajiwa kukamilika Juni 30 mwaka huu ambapo awali fedha iliyopokelewa na Manispaa hiyo ilikuwa ni zaidi ya shilingi bilioni saba ambayo imeanza kutekeleza mradi huo ambapo hadi sasa mkandarasi husika amekwisha lipwa kwanza shilingi bilioni nne.


Alifafanua kuwa barabara za Manispaa ya Songea ambazo zipo kwenye mradi huo ni kuanzia maeneo ya mtaa wa FFU hadi Matogoro yenye urefu wa kilometa 3.2, barabara ya Songea Girl’s hadi Mateka yenye urefu wa kilometa 1.5 na barabara ya Mwembechai hadi Bombambili yenye urefu wa kilometa 2.6.

Midelo aliongeza kuwa nyingine ni ya kutoka mtaa wa Mitumbani hadi Yapenda yenye urefu wa kilometa moja, barabara ya Polisi hadi Stendi ya Mlilayoyo yenye urefu wa kilometa 0.45.


Hata hivyo muda wa kumaliza kazi kwa Mkandarasi ulikuwa ni tangu mwezi Juni 30 mwaka huu ambapo kufuatia hali hiyo tayari Mkandarasi huyo ameingizwa kwenye tozo (Liquidated Damage) na kwamba iwapo atashindwa kumaliza kazi kwa siku 100 hatua za kisheria za kuvunja mkataba wake zitafanyika.

No comments: