Wednesday, August 9, 2017

MANISPAA YA SONGEA WAPO HATARINI KUUGUA MAGONJWA YATOKANAYO NA MIFUGO


Mkaguzi wa mifugo katika machinjio ya Msamala Manispaa ya Songea, Angela Mbata upande wa kulia akiwaonesha juzi baadhi ya wananchi waliofika kwenye banda hilo la mifugo la nyama ya ng'ombe zilizopatwa na magonjwa mbalimbali ikiwemo majipu kwenye ini na mapafu ambayo endapo binadamu akila kuna hatari kubwa ya kuambukizwa magonjwa hayo.
Na Muhidin Amri,      
Songea.

IMEELEZWA kuwa wakazi wa Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wapo hatarini kuugua magonjwa yatokanayo na mifugo ikiwemo ugonjwa wa majipu na TB baada ya kubainika kwamba, baadhi ya wafanyabiashara wachache wamekuwa wakichinja na kuuza nyama bila kukaguliwa na madaktari wa mifugo.

Hayo yalisemwa juzi na mkaguzi wa mifugo katika machinjio ya Msamala katika Manispaa hiyo, Angela Mbata wakati alipokuwa akitoa elimu ya mifugo na umuhimu wa kula nyama iliyopimwa kwa wananchi waliohudhuria kwenye maonesho ya wakulima maarufu kwa jina la nanenane mkoani hapa yaliyofanyika katika kata ya Masamala.

Mbata alifafanua kuwa uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa ng’ombe 15 kati ya 30 wanaoletwa na wafugaji mkoani humo kutoka katika mikoa mbalimbali kwa ajili ya kuchinjwa, imebainika kuwa na ugonjwa wa minyoo kwenye ini na mapafu ambayo husababisha majipu jambo ambalo ni hatari kubwa kwa walaji.


Alisema kuwa binadamu atakayekula nyama hasa maini na mapafu ya wanayama waliokuwa na ugonjwa huo ni rahisi na yeye kuambukizwa na kwamba tatizo hilo linatokana na mifugo kutotibiwa kwa muda mrefu hasa ile inayotoka kwenye mnada wa Mbeya ambapo wafugaji wanasafirisha mifugo yao kupitia njia za panya.

Aidha aliongeza kwa kuwatahadharisha wananchi kuwa makini na kuepuka kununua na kula nyama mitaani kwa sababu mifugo inayochinjwa katika maeneo yao wakati mwingine sio salama kwa kuwa haikaguliwi na madaktari wa mifugo wakiwa na lengo la kuepuka gharama.

Alibainisha kuwa katika kuwanusuru wananchi waishi katika Manispaa ya Songea wamejipanga kuhakikisha mifugo yote inayoingia ikitoka nje ya Manispaa hiyo ni lazima ikaguliwe kwanza, kabla ya kupeleka kwenye minada kwani wasipofanya hivyo inaweza kuleta madhara makubwa kwa binadamu na hatimaye kushindwa kushiriki vyema katika shughuli za ujenzi wa taifa.

Kadhalika alisema serikali imejipanga kuhakikisha kwamba hakuna ng’ombe atakayechinjwa bila kukaguliwa na daktari ambapo mfugaji au mfanyabiashara yeyote atakayeingiza au kuuza nyama isiyopimwa atapewa adhabu kali ikiwemo kufikishwa Mahakamani kupigwa faini na kwenda kutumikia kifungo jela.


Hata hivyo Mbata alibainisha kuwa tatizo la wananchi hasa wakulima wa mkoa wa Ruvuma ni kutopenda kuhudhuria na kushiriki kikamilifu maonesho mbalimbali ya wakulima ambayo yanaweza kuwasaidia kupata elimu kuhusu ufugaji wa kisasa, kilimo bora na ulaji wa vyakula unaozingatia kanuni bora za afya.

No comments: