Sunday, August 6, 2017

WANACHAMA WA MBINGA WALIMU SACCOS WAKUBALIANA WALIOSHIRIKI KUHUJUMU CHAMA NA KUSABABISHA HASARA WAFIKISHWE MAHAKAMANI

Wanachama wa chama cha ushirika Mbinga walimu SACCOS wakiwa katika mkutano wao maalumu uliofanyika jana kwenye ukumbi wa jumba la maendeleo uliopo Mbinga mjini mkoani Ruvuma, wakijadili juu ya urejeshaji wa fedha zao zilizotumika vibaya katika utoaji wa mikopo hewa inayodaiwa kutolewa na viongozi wa bodi na watendaji waliopita katika ushirika huo jambo ambalo limesababisha chama chao kushindwa kujiendesha ambapo walifikia maazimio kwamba wahusika wachukuliwe hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani. 
Judith Komba ambaye ni mmoja kati ya wajumbe wa bodi ya mpito ya chama cha ushirika Mbinga Walimu SACCOS akisoma taarifa jana juu ya matumizi mabaya na mikopo hewa ya fedha ambayo inadaiwa kutolewa na viongozi wa bodi na watendaji waliopita na kusababisha chama hicho kupata hasara huku kikishindwa kujiendesha kwa manufaa ya wanachama wake. Aliyekaa katikati ni Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye na wa kwanza upande wa kulia ni Mwenyekiti wa bodi ya mpito ya chama hicho Vitalis Mapunda.
Aliyesimama ni Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Cosmas Nshenye akisisitiza jambo jana kwenye mkutano maalum wa chama cha ushirika Mbinga Walimu SACCOS ambapo alisema kuwa wahusika waliochukua fedha za ushirika huo bila kufuata taratibu husika wasipozirejesha mapema Ofisi yake itachukua hatua kali za kisheria, kutoka kushoto ni Wernery Mhagama ambaye ni Katibu wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Mbinga na wapili ni Batson Mpogolo ambaye ni Mwenyekiti wa CWT wilayani humo. 
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

CHAMA cha ushirika Mbinga Walimu SACCOS kilichopo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma kimepata hasara ya shilingi bilioni 1,033,002,579 ambazo zilitokana na akiba, hisa na amana za wanachama jambo ambalo hivi sasa limesababisha chama hicho kushindwa kujiendesha kwa manufaa ya wanachama wake.

Aidha kufuatia hali hiyo wanachama hao wamekubaliana kwamba viongozi wa bodi na watendaji wake walioshiriki kukihujumu na kusababisha hasara hiyo wachukuliwe hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani ili waweze kulipa fedha hizo.

Makubaliano hayo ya wanachama hao yalifikiwa katika mkutano wao maalumu ulioketi jana kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa mbele ya mgeni rasmi Mkuu wa wilaya hiyo, Cosmas Nshenye.

Akisoma taarifa ya ukaguzi ya SACCOS hiyo mbele ya Mkuu huyo wa wilaya mmoja kati ya wajumbe wa bodi ya mpito ambayo iliteuliwa kwa muda kusimamia na kuongoza chama hicho, Judith Komba alisema kuwa mpaka kufikia Septemba 26 mwaka jana chama ilibidi kiwepo na fedha hizo lakini hakina fedha kutokana na matumizi mabaya yaliyokuwa yakifanyika na viongozi wa bodi na watendaji wake waliokuwepo hapo awali.


Alifafanua kuwa fedha hizo ambazo wanadaiwa kujinufaisha kwa matakwa yao binafsi zimetokana na akiba za wanachama ambazo zilitakiwa kuwepo shilingi milioni 929,091,579, hisa shilingi milioni 90,760,000 na amana shilingi milioni 13,151,000 lakini kumekuwa na mbinu chafu ambazo zilikuwa zikitumika kutengeneza mikopo hewa isiyofuata taratibu ndiyo maana hasara hiyo imejitokeza ndani ya chama.

Komba alieleza kuwa bodi hiyo na watendaji hao wamesababisha pia mikopo hiyo kutolewa bila kujali hisa na akiba alizonazo mwanachama hivyo kusababisha hata mkopo husika kushindwa kurejeshwa kupitia makato yanayokatwa katika mfumo unaozingatia theluthi tatu ya mshahara wa mkopaji.

Naye Mwenyekiti wa bodi hiyo ya mpito Mbinga Walimu SACCOS, Vitalis Mapunda aliwataja wanaonyoshewa kidole wakidaiwa kuhusika juu ya upotevu wa fedha hizo za wanachama kuwa ni Sostenes Ndunguru ambaye alikuwa Meneja, Stephen Komba mjumbe kamati ya usimamizi na Edmund Hyera ambaye alikuwa ni mjumbe wa bodi.

Vilevile wengine ni Emmanuel Kapinga aliyekuwa Mwenyekiti, Kenneth Ndunguru, John Komba, Peter Challe, Batson Mpogolo, Osmund Komba, Wille Mkwene, Marion Nchillas, Materinus Ndunguru na Tabu Mshani, Menas Matembo, Gervas Kapinga, Osmund Kihwili, Salvanus Hyera, Samwel Maridadi, Mary Nchimbi na Sadick Mango ambao wote nao walikuwa ni wajumbe wa bodi katika SACCOS hiyo.

Awali kwa upande wake akizungumza katika mkutano huo Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Nshenye alisema kuwa yeye ofisi yake haitaweza kuvumilia vitendo hivyo vya wizi wa fedha za wananchama hao na kwamba amewataka wale wote waliohusika kuchukua fedha hizo bila kufuata taratibu wazirejeshe mapema iwezekanavyo kabla hawajachukuliwa hatua kali za kisheria.

“Mimi sina hiyo huruma kwa sababu kama umevunja sheria haijalishi wewe ni mtumishi au sio mtumishi, kwangu hawa wahalifu siwahitaji mimi natoa agizo watafutwe popote walipo waitwe walipe fedha hizi kabla hatua nyingine hazijachukuliwa”, alisisitiza Nshenye.

Kadhalika kufuatia kuwepo kwa hali hiyo pia Nshenye alitoa onyo kwa viongozi na watendaji wa vyama vya ushirika wilayani humo kuacha mara moja vitendo vya wizi wa fedha na mali za ushirika.

Nao wakichangia hoja kwa nyakati tofauti katika mkutano huo wanachama wa SACCOS hiyo waliunga mkono jitihada hizo wakisema kuwa wale wote ambao wanadaiwa na chama hicho wakamatwe na endapo kama wanakaidi kurejesha fedha hizo wachukuliwe hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa mahakamani.

Walisema wamesikitishwa na taarifa hizo ambazo zinaonesha kuwa ni utovu mkubwa wa nidhamu uliofanyika ndani ya chama chao juu ya matumizi mabaya ya fedha za wanachama.

Inosensia Nombo ambaye ni mmoja kati ya wanachama wa ushirika huo aliongeza kuwa taarifa hiyo ya ukaguzi ambayo ilisomwa mbele yao inaonesha kuwa na ubadhirifu mkubwa wa fedha na dosari nyingi za kiutendaji, hivyo kuna kila sababu kwa viongozi waliohusika kuchukuliwa hatua ili iweze kuwa mfano na fundisho kwa wengine.

Pia Gerald Ndunguru naye alisema; “wakati najiwekea akiba mpaka nafikia hatua ya kustaafu haki zangu sijazipata kwa kilio hiki kilichotupata, hawa watuhumiwa wanastahili kabisa kukamatwa na kutiwa pingu mikononi ili wafikishwe mahakamani kwani inasikitisha na kutuongezea uchungu mkubwa katika maisha yetu”.


Hata hivyo pamoja na mambo mengine, chama cha ushirika Mbinga Walimu SACCOS kinaundwa na wanachama ambao ni watumishi wa serikali wanaotoka katika halmashauri ya mji wa Mbinga, wilaya ya Mbinga na Nyasa ambapo makao makuu ya ofisi zake yapo Mbinga mjini.

No comments: