Tuesday, June 2, 2015

MADAKTARI BINGWA WAPONGEZWA KWA KUTIBU WAGONJWA WENYE MAGONJWA SUGU TUNDURU

Na Steven Augustino,
Tunduru.

WAGONJWA 63 kutoka wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, wameripotiwa kufanyiwa upasuaji mkubwa na Madaktari bingwa, kutoka Hospitali mbalimbali Jijini Dar es Salaam na KCMC iliyopo mkoani Kilimanjaro.

Mganga mkuu wa hospitali ya wilaya hiyo, Dokta Alex Kazula alisema hayo alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake na kuongeza kuwa katika matibabu hayo madaktari hao, pia waliwafanyia uchunguzi wagonjwa 171 ambapo kati yao wengine walipewa ushauri na wengine kufanyiwa matibabu.

Alieleza kuwa zaidi ya wagonjwa 200 walishindwa kuonana na wataalamu hao kutokana na muda wao kwisha, pamoja na wodi za hospitali ya wilaya hiyo kujaa na kukosekana na nafasi ya kuwahifadhi.


Dokta Kazula alisema wagonjwa waliopatiwa tiba ni pamoja na wale ambao walikuwa wakisumbuliwa na tezi ya shingo (Goita), ngiri, kidole tumbo na uvimbe katika mji wa uzazi.

Aidha magonjwa ambayo walikosa huduma ya matibabu kutokana na kukosekana kwa vipimo husika, ni pamoja na wagonjwa wenye kansa mbalimbali na kwamba wazo la kuwaleta madaktari hao bingwa lilitokana na idara yake, kutambua uwepo wa mahitaji makubwa ya matibabu kutoka kwa wananchi wa Tunduru ambao wengi wao, husumbuliwa na magonjwa sugu kwa muda mrefu.

Vilevile alisema wataalamu hao, ni mabingwa wa kufanya upasuaji na tiba hasa kwa magonjwa ya wanawake ambapo juhudi za kuwaleta ni mpango ambao ulifanywa na serikali kutokana na wilaya hiyo, kuwa pembezoni karibu na nchi ya Msumbiji na watu wengi husumbuliwa na magonjwa hayo.


Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Chande Nalicho alipongeza jitihada zilizofanywa na madaktari hao kwa kutoa huduma hiyo ya matibabu kwa gharama nafuu, kwa watu ambao uwezo wao wa kifedha upo chini.

No comments: