Saturday, June 27, 2015

MFUGAJI ASHAMBULIWA NA SIMBA TUNDURU

Na Steven Augustino,
Tunduru.

MFUGAJI mwenye asili ya Mmang’ati, ambaye ametambuliwa kwa jina la Alex Poketi (22) amelazwa katika Hospitali ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, baada ya kujeruhiwa vibaya na simba wakati akiwa machungani.

Walioshuhudia tukio hilo, walisema kuwa majeruhi huyo alipatwa na mkasa huo wakati akijitosa kuokoa maisha ya ng’ombe wake ambao walivamiwa na mnyama huyo mkali, kwa lengo la kutaka kuwafanya kitoweo.

Walisema tukio hilo lilitokea katika kijiji cha Mbuyuni kilichopo kando kando ya mto Ruvuma, eneo ambalo wafugaji hao wamekuwa wakichungia mifugo yao tangu mwaka 2007.

Katika eneo hilo imeelezwa kuwa, simba huyo alijitokeza ghafla na kuanza kushambulia ng’ombe hao aliokuwa akiwachunga ambapo Alex alijawa na jazba na kwenda kumrukia simba huyo kwa kumchoma mkuki, jambo ambalo lilimfanya mnyama huyo akimbie.


Wakati hilo likifanyika, ghafla simba huyo alijitokeza tena kwa mara ya pili na kuanza kumshambulia kijana huyo kwa kumkwaruza na kucha zake sehemu mbalimbali za mwili wake, hali ambayo ilimsababishia majeraha makubwa.

Mganga mfawidhi wa hospitali ya wilaya ya Tunduru, Dokta Mmari Zabron alikiri kumpokea majeruhi huyo na kuongeza kuwa wamefanya jitihada ya kumpatia matibabu kwa kumshona nyuzi, sehemu ambazo zina majeraha makubwa.

Alifafanua kuwa majeruhi huyo ana hali mbaya kwani bado hajitambui kutokana na kuumizwa vibaya sehemu ya kifuani, mikononi na katika mapaja ya miguu yake.


Japhet Mnyagala ambaye ni ofisa ardhi na maliasili wilayani humo, alisema tayari amekwisha tuma kikosi cha askari wenye silaha kwa ajili ya kwenda kumsaka simba huyo kwa lengo la kumuua, ili asiweze kuleta madhara mengine makubwa kwa wananchi hapo baadaye.

No comments: