Tuesday, June 2, 2015

WANAFUNZI VYUO VYA ELIMU WATAKIWA KUREJESHA MIKOPO KWA WAKATI

Wahitimu wa chuo cha sayansi na tekinolojia cha Mtakatifu Joseph mjini Songea mkoani Ruvuma, wakiwa wamekaa katika picha ya pamoja.
Na Julius Konala,
Songea.

WANAFUNZI wanaosoma katika vyuo vya elimu ya juu hapa nchini, wamekumbushwa kurejesha mikopo yao kwa wakati ambayo ilitolewa na serikali kupitia Bodi ya mikopo ya wanafunzi hapa nchini, kadiri ya makubaliano yaliyofanywa kwenye mikataba yao ili iweze kusaidia wengine.

Mkurugenzi anayeshughulikia urejeshaji mikopo katika bodi hiyo, Juma Chagonja alisema hayo alipokuwa akizungumza na wahitimu wa chuo cha sayansi na tekinolojia ya mawasiliano, cha Mtakatifu Joseph mjini Songea mkoani Ruvuma.

Alisema kwamba bodi imefikia maamuzi hayo, baada ya kuona baadhi ya wanafunzi ambao wamenufaika na mkopo husika kuwa wagumu katika kurejesha ingawa wapo kwenye ajira, huku akiongeza kuwa wanapaswa kutambua kuwa haikutolewa kama zawadi.


Chagonja alifafanua kuwa kitendo hicho imekuwa ni tatizo kubwa kwa bodi, kwa kile alichoeleza kuwa hivi sasa wanashindwa kuendelea na mzunguko wa kutoa mikopo kwa wanafunzi wengine, ambao wamejiunga na vyuo hivyo kutokana na ukosefu wa fedha ambazo nyingi bado zipo mikononi mwa wahitimu wa vyuo.

Kufuatia hali hiyo uongozi husika wa bodi ya mikopo hapa nchini, umeamua kutoa stetimenti za mikopo kwa wahitimu hao ikiwa ni sehemu ya kuwakumbusha kurejesha mikopo yao kwa muda muafaka, ambayo walikopeshwa na serikali.


Mkurugenzi huyo alisema kuwa katika kukabiliana na changamoto hiyo, hatua mbalimbali zimechukuliwa ikiwemo vyeti vyote vya wanufaika wa mikopo vitakuwa na udhamini wa mhitimu kwa lengo la kumrahisishia, mwajiri wake kuwasiliana na bodi kwa ajili ya kuangalia utaratibu wa urejeshwaji pale anapoajiriwa.

No comments: