Friday, June 26, 2015

TASAF TUNDURU YAWATAKA WANANCHI KUTOA USHIRIKIANO


Baadhi ya Wataalamu kutoka katika kata mbalimbali wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wakiwa katika semina ya mpango wa TASAF kwa ajili ya kwenda kutoa elimu kwa wananchi vijijini.

Na Steven Augustino,

Tunduru.

WANANCHI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wameombwa kutoa ushirikiano wa kutosha juu ya hatua zote zinazotakiwa kutekelezwa pale unapofanyika upembuzi yakinifu katika matatizo yao, hasa yale yanayolenga uhifadhi wa udongo, uvunaji maji, udhibiti makorongo na kuotesha vitalu vya miti.

Aidha wametakiwa kuondokana na dhana potofu ambazo zinaenezwa na watu wasio na nia njema, kwa yale yanayofanywa katika awamu ya tatu ya utekelezaji wa mpango wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wakiwa na lengo la kutaka kukwamisha maendeleo ya mpango huo, ili usiweze kuleta mafanikio katika jamii wilayani humo.

Hayo yalisemwa na Peter Lwanda ambaye ni mmoja kati ya watendaji wa mfuko huo, alipokuwa akimwakilisha Mkurugenzi mtendaji wa TASAF hapa nchini, Ladislaus Mwamanga akitoa maelezo ya kuutambulisha juu ya kutoa ajira za muda, kupitia mpango wa kunusuru kaya maskini kwenye kikao cha kazi kilichofanyika ukumbi wa Klasta ya walimu tarafa ya mlingoti mjini hapa.


Lwanda alifafanua kuwa mpango huo, unafuatia uzinduzi uliofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete Agosti 15 mwaka 2012 na kuanza kutekelezwa mwaka 2013 ukilenga kunusuru kaya maskini kwa kuziwezesha kupata huduma muhimu hasa katika nyanja ya elimu, afya na maji.

Alisema mpango huo unatekelezwa kwa kipindi cha miaka kumi, na kwamba kaya milioni moja zinazoishi hapa nchini, katika mazingira duni ya umaskini zitafikiwa na kuwezeshwa.

Mpango huo wenye sehemu kuu tano, ikiwemo ya uhawilishaji fedha kwa kutoa ruzuku katika kaya hizo ambazo zina watu wenye uwezo wa kufanya kazi, kujenga na kuboresha miundombinu inayolenga katika sekta husika na kujenga uwezo katika ngazi zote za utekelezaji.

Kadhalika mpango huo unatekelezwa na serikali pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo, wanaochangia wakiwemo Benki ya dunia, Shirika la Maendeleo la kimataifa la Sweeden (SIDA), Mpango wa maendeleo ya umoja wa mataifa (UNDP), Shirika la umoja wa mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) pamoja na Shirika la kazi la umoja wa mataifa (ILO).

Naye Fadhil Mshamu ambaye alikuwa akimwakilisha Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Tunduru, Faridu Khamis TASAF katika mpango huo wa awamu ya tatu pia alieleza kuwa unalenga kaya maskini zenye watoto chini ya miaka kumi na akina mama wajawazito waweze kupata lishe bora, huduma za afya, elimu, maji ikiwemo na ajira kwa kupitia ruzuku za aina mbili, ya msingi na ya kutimiza masharti maalumu.

Washiriki 48 kutoka kata mbalimbali wilayani humo, wamepatiwa mafunzo juu ya utekelezaji wa mpango huo ambao walikuwa wakitoka katika makundi ya wataalamu wa miundombinu ya maji, kilimo, umwagiliaji, afya, elimu, mazingira na uvuvi ili baadaye huko waendako wakasaidie kuelimisha wananchi katika maeneo yao juu ya utekelezaji wake.

No comments: