Tuesday, June 9, 2015

PADRI ALIYEFARIKI AJALINI AZIKWA

Gari hili ndilo walilopata nalo ajali Wanafunzi na Padri wa kanisa katoliki jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAUMINI wa madhehebu mbalimbali ya dini wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wameshauriwa kuwa watulivu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi, kufuatia ajali ya gari lililoteketea kwa moto na kusababisha baadhi ya wanafunzi na Padri wa kanisa katoliki wilayani humo, kufariki dunia.

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Mbinga, John Ndimbo wakati alipokuwa akiongoza ibada ya mazishi ya Padri Hyasint Kawonga ambaye alifariki dunia, kwenye ajali hiyo na kusababisha vifo vya watu saba wakiwemo wanafunzi sita, Padri huyo na majeruhi 24.

Wanafunzi wanaosoma katika shule ya Kigonsera Catechists Secondary School (KCS) iliyopo katika kata ya Kigonsera, akiwemo na Padri Kawonga ambaye ni Mkurugenzi wa shule hiyo, Parokia ya Kigonsera katika jimbo hilo walipoteza maisha baada ya gari walilokuwa wakisafiria, kutumbukia kwenye korongo na kuteketea kwa moto.


Askofu Ndimbo alisema katika kipindi hiki cha majonzi na maombolezo, kuna kila sababu ya waumini wa kikristo kuendelea kuwaombea marehemu hao kwa kusali na kumuomba Mungu, azilaze roho zao mahali pema peponi.

Ibada hiyo ya mazishi ilihudhuriwa na mamia ya watu wakiwemo na viongozi wa dini kutoka sehemu mbalimbali ndani na nje ya mkoa wa Ruvuma, ambapo mwili wa marehemu Kawonga umelazwa katika makaburi ya Parokia ya Kigonsera wilayani Mbinga.

Kadhalika nao wanafunzi waliofariki ambao walikuwa wanasoma katika shule hiyo ya KCS ambao ni Fidea Ndunguru(17) na Suzan Kawonga (17) wote wa kidato cha nne miili yao ilisafirishwa kwenda katika kijiji cha Mpapa wilayani Mbinga kwa ajili ya mazishi.

Wengine wawili walisafirishwa kwenda makwao ambao ni wa familia moja walikuwa wakisoma kidato cha nne ni wa kutoka kijiji cha Namabengo wilaya ya Namtumbo, ambao ni Gladness Ngonyani (17) na Kelvin Ngonyani (20) na kwamba Damas Mbele (16) wa kidato cha pili kutoka kijiji cha Myanga yanga na Philoteus Hyera (16) kijiji cha Mahenge ni wa kutoka wilayani Mbinga nao walisafirishwa kwenda nyumbani kwao kwa ajili ya mazishi.

Pamoja na mambo mengine, Kamati ya ulinzi na usalama wilayani Mbinga, ikiongozwa na Mwenyekiti wake ambaye ni Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga ilitoa masanduku saba ya kuzikia pamoja na gharama za usafiri.

Awali kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela alipozungumza na mwandishi wa habari hizi alifafanua kuwa ajali hiyo ilitokea Juni 4 mwaka huu majira ya jioni, wakati Wanafunzi hao na Padri Kawonga walipokuwa wakitoka shambani kuvuna mahindi yaliyokuwa yamelimwa kwa ajili ya chakula cha wanafunzi shuleni hapo.


Padri Kawonga ndiye aliyekuwa akiendesha gari hilo ambalo lilipata ajali lenye namba za usajili T 306 AYM aina ya Land rover, One ten baada ya kushindwa kupanda mlima katika eneo la Minazi kata ya Kigonsera ndipo lilirudi nyuma na kutumbukia kwenye korongo kisha kuwaka moto huku ndani ya gari, wakiwa wanafunzi na padri huyo ambao waliteketea kwa moto.

No comments: