Saturday, June 6, 2015

TUWEMACHO TUNDURU KUJENGEWA ZAHANATI NA TASAF

Na Steven Augustino,
Tunduru.

MFUKO wa maendeleo ya jamii (TASAF) awamu ya tatu ambao kwa sasa unatekeleza mradi wa uhawilishaji fedha kwa kaya maskini hapa nchini, umeridhia ombi la kugharimia ujenzi wa zahanati, katika kijiji cha Tuwemacho wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma.

Hayo yamefuatia baada ya makubaliano yaliyofanyika, kati ya viongozi wa mfuko huo na wananchi walioshiriki kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo, ambao ulilenga kuibua mradi huo na ujenzi wake kugharimu zaidi ya shilingi milioni 75.

Kwa mujibu wa wananchi waliokuwepo katika mkutano huo, kwa nyakati tofauti walipendekeza pia wajengewe mradi wa maji, nyumba za walimu, vyumba vya madarasa, matundu ya choo na ghala la kuhifadhia mazao.


Akizungumzia juu ya makubaliano hayo Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Tunduru, Tina Sekambo ambaye naye alishiriki katika mkutano huo aliwataka wananchi hao wakati wa utekelezaji wa mradi huo, washiriki kikamilifu kuchangia asilimia 10 wakati utekelezaji wake utakapoanza.

Sambamba na kuwepo kwa utaratibu huo, Sekambo aliwataka kufanya mkutano mwingine wa hadhara kwa siku zijazo, kwa lengo sasa kujenga makubaliano wapi mradi utajengwa na kufanya makubaliano ya pamoja, kutafuta eneo ambalo halina mgogoro na halitahitaji kulipwa fidia.


Naye mshauri wa mfuko wa TASAF wilayani Tunduru, Christian Amani aliwahakikishia wananchi hao kuwa utekelezaji wa mradi huo ujenzi wa zahanati utaanza kutekelezwa mapema iwezekanavyo, mara baada ya taratibu husika kukamilika.

No comments: