Friday, June 26, 2015

NJOWOKA KUMALIZA KERO YA UJENZI ZAHANATI NKALACHI NYASA

Wananchi wa kijiji cha Nkalachi kata ya Liuli wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, wakiwa wamemzunguka na kumsikiliza kwa makini Kamanda wa Umoja wa Vijana wa Chama cha mapinduzi (UVCCM) wa wilaya hiyo, Cassian Njowoka wakati alipokuwa akiwahutubia.
Na Kassian Nyandindi,
Nyasa.

WANANCHI wanaoishi katika kijiji cha Nkalachi kata ya Liuli wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, wameiomba serikali na wadau mbalimbali wasaidie vifaa vya kiwandani ili waweze kukamilisha ujenzi wa jengo la Zahanati ya kijiji hicho na hatimaye waondokane na kero ya kukosa huduma za matibabu.

Aidha walisema kuwa hivi sasa akina mama wajawazito na watoto wadogo wamekuwa wakifariki dunia, hasa pale wanapokuwa njiani kuelekea Hospitali ya Anglikana iliyopo wilayani humo, ambayo ipo mbali nao kwa ajili ya kutafuta matibabu.

Hayo yalisemwa kwa nyakati tofauti na wakazi wa kijiji hicho, mbele ya Kamanda wa Umoja wa vijana wa chama cha mapinduzi (UVCCM), Cassian Njowoka walipokuwa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini humo.


“Sisi wananchi tumeanza kazi ya ujenzi wa jengo la zahanati yetu ya kijiji, tunawaomba wadau mbalimbali watusaidie kutoa mchango wao wa vifaa vya kiwandani ili tuweze kukamilisha ujenzi wa jengo hili, akina mama wengi wajawazito wanapoteza maisha wakati wa kujifungua kutokana na kukosa huduma za kitabibu”, walisema.

Kwa upande wake Kamanda UVCCM wilaya ya Nyasa, Njowoka baada ya kusikiliza kilio hicho cha wakazi wa kijiji cha Nkalachi aliweza kutoa ahadi ya kuchangia vifaa hivyo vya kiwandani, ikiwemo bati, nondo, mifuko ya saruji, vitanda vya kujifungulia akina mama wajawazito pamoja na gharama za kulipa mafundi ambao wanaendelea na kazi hiyo ya ujenzi.


“Ndugu zangu nitachangia vifaa vyote vya kiwandani mpaka jengo hili litakapofikia hatua ya kukamilika ujenzi wake, naiomba kamati husika ya ujenzi iketi chini na kufanya tathimini juu ya gharama hizi za ujenzi na baadaye mniletee niweze kukamilisha”, alisema Njowoka.

No comments: