Wednesday, June 10, 2015

UTEKELEZAJI WA TASAF TUNDURU WADAIWA KUWA MWIBA KWA WANUFAIKA

Na Steven Augustino,
Tunduru.

TAARIFA potofu kuhusu utekelezaji wa mpango wa uhawilishaji fedha ili kuziwezesha kaya maskini kujikimu kiuchumi, unaotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) awamu ya tatu wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, unadaiwa kuendelea kuwa mwiba kwa wanufaika hali ambayo inawafanywa kushindwa kubuni mikakati ya kujiendeleza, kupitia mfuko huo.

“Ingawa wataalamu wetu wamekuwa wakitupatia elimu ya kujikwamua na umaskini kupitia vikundi vyetu vya ujasiriamali, ambavyo tunawekeza katika vikundi vya Mpeano miongoni mwetu wamekuwa wakiogopa kujiunga na vikundi hivi kutokana na kuhofia kuwa huenda mpango huo, utakwisha kabla hawajamaliza mzunguko wa mpeano wao kwa sababu chanzo ni uwepo wa taarifa potofu hivyo familia zao kukosa uwezeshaji huo”, walisema.

Hayo na mengine mengi yalibainika kufuatia uchunguzi uliofanywa na mwandishi wetu, wakati waratibu husika wa mpango huo wilayani humo wakiwajibika kuelimisha wananchi wakati wa malipo ya fedha, kwa walengwa waliokuwemo kwenye mpango huo katika vijiji vilivyomo wilayani humo.


Halima Chipala, Zaina Chipande na Fatu Chingulu kutoka kijiji cha Mchoteka wilayani Tunduru, ni kati ya wanufaika waliotoa ukimya huo baada ya kuwahoji wataalamu hao na kuongeza kuwa wengi wa wanufaika hao wamekuwa wakipotoshwa na wananchi ambao hawapo kwenye mpango huo, kuwa endapo wataanzisha vikundi hivyo vya mpeano ipo hatari miongoni mwao kutonufaika na huduma husika.

Mbali na kuwepo kwa baadhi ya wanufaika wachache ambao wamesema hivi sasa wameanza kujipanga kuunda vikundi vya uzalishaji mali, ikiwemo kununua mifugo aina ya kuku, bata na mbuzi ili baadaye waifuge lakini hali halisi ya utekelezaji inaonekana kuwa na changamoto nyingi zinazohitaji walengwa, kupewa elimu ya kutosha ili kuondokana na tatizo hilo.

Wengi wa wanufaika wameonekana kuipongeza serikali, kwa kubuni mpango huo ambapo wameonesha kuanza kuwekeza fedha walizopata ili hapo baadaye ziweze kuwasaidia pale mradi utakapofikia kikomo.

Mzee Mustapha Tawakali na Khadija Mussa kutoka kijiji cha Mkasale tarafa ya Namasakata wilayani humo, walisema kutokana na upotoshwaji huo kuna kila sababu ya kuona kwamba wananchi inawafikia elimu ya kutosha ipasavyo, ili hali hiyo isiweze kuendelea kuwepo miongoni mwa jamii.

Taarifa zilizotolewa na Mkurugenzi mtendaji wa TASAF, Ladislaus Mwamanga alisema mpango huo ulizinduliwa na Rais Jakaya Kikwete Agosti 15 mwaka 2012 na kuanza kutekelezwa Februari 2013 unalenga kunusuru kaya maskini, kwa kuzisaidia fedha ili ziweze kupata huduma mbalimbali ikiwemo katika sekta ya elimu, afya na maji.

Kupitia mpango huo ambao utekelezaji wake ni wa miaka kumi, utazinufaisha kaya milioni moja zinazoishi katika mazingira duni ya umaskini zitafikiwa na kuwezeshwa kupitia mgawanyo wa sehemu kuu tano, ikiwemo ya uhawilishaji fedha kwa kutoa ruzuku kwa kaya maskini zenye watu wenye uwezo wa kufanya kazi kujenga na kuboresha miundombinu husika inayolenga katika sekta hizo.


Taarifa hiyo inafafanua kuwa mpango huo utawezesha pia kaya zenye watoto chini ya miaka mitano na akina mama wajawzito, ikilenga kuwapatia lishe bora, huduma za afya, elimu, maji na ajira kupitia ruzuku za aina mbili ya msingi na ya kutimiza masharti maalum.

No comments: