Thursday, June 18, 2015

MBESA TUNDURU WAPO HATARINI KUUGUA HOMA ZA MATUMBO

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

UKOSEFU huduma ya uhakika ya upatikanaji wa maji safi na salama, katika kijiji cha Mbesa wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kuna hatarisha wakazi wa kijiji hicho kuugua homa ya matumbo, kipindupindu na kuhara kutokana na kunywa maji machafu.

Zaidi ya wakazi 7,000 wanaoishi huko, wapo hatarini kukumbwa na madhara hayo ambapo licha ya serikali kuweka katika mpango wa ujenzi wa mradi wa maji ambao utagharimu shilingi milioni 700, utekelezaji wake mpaka sasa unaonekana ukisuasua na kuwafanya wananchi wajenge hofu juu ya usalama wa maisha yao.

Wananchi wa kijiji cha Mbesa, walipozungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti walisema kuwa kutokana na kuwepo kwa tatizo hilo wamekuwa wakinywa maji machafu yaliyopo kwenye vyanzo ambavyo hata wanyama wakali kama vile simba, tembo, chuwi na nyoka wakubwa wamekuwa wakinywa maji hayo jambo ambalo linawafanya waishi kwa hofu kubwa.

Awanda Yusuph na Zuhura Said walisema kuwa katika kipindi cha mwaka 2013 walianza kupata matumaini baada ya serikali kupitia mradi mkubwa, ambao unatekelezwa kwa ufadhili wa benki ya dunia na kumpatia kazi hiyo mkandarasi wa kampuni ya Nyakile Investment Company Limited, lakini utekelezaji wake mpaka sasa haujazaa matunda.


Afisa mtendaji wa kijiji hicho, Ally Mchonjele amethibitisha kwamba kijiji chake kina jumla ya wakazi 7,846 huku akikiri kuwa ni kipindi kirefu sasa kimepita wamekuwa wakitumia maji, kutoka kwenye visima vya kienyeji ambayo sio salama kwa afya ya binadamu.

Diwani wa kata ya Mbesa, Shaibu Kamtiko pamoja na kuonesha mashaka juu ya ukamilishaji ujenzi wa mradi huo alisema wananchi walikuwa wakitegemea kunywa maji kutoka kwenye visima 21 ambavyo vilichimbwa miaka ya 1980 na hivi sasa visima vitatu tu, ndivyo vinavyofanya kazi hali ambayo inasababisha kutopatikana kwa huduma hiyo muhimu.

Mhandisi kutoka idara ya maji wilayani Tunduru, Emmanuel Mfinanga pamoja na kukiri kuyumba kwa maendeleo ya mradi huo alisema tayari idara hiyo inafanya utaratibu wa kuvunja mkataba na mkandarasi huyo, kutokana na ubabaishaji uliojitokeza katika utekelezaji wake.

Mfinanga alifafanua kuwa miongoni mwa maelekezo aliyopatiwa mkandarasi huyo ni pamoja na kuhakikisha kwamba, anapeleka wataalamu wa kutosha ambao wataweza kuendelea na ujenzi huo, kitendo ambacho utekelezaji wake umekuwa hafifu.

Akizungumzia juu ya hali hiyo Mkurugenzi mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Tunduru, Tina Sekambo pamoja na kukiri juu ya matatizo hayo katika mradi huo alisema halmashauri ipo katika harakati za kutafuta ufumbuzi wa kudumu ili kumaliza kero hiyo, ambayo inawakabili wananchi wa kijiji hicho.

Sekambo alieleza kuwa mradi huo ulipangwa kugharimu jumla ya shilingi milioni 716,539,050 na kukamilika Februari mwaka huu, na kwamba kati ya fedha hizo tayari mkandarasi amekwisha lipwa milioni 473 kwa ajili ya ujenzi wa tanki na banio.

No comments: