Tuesday, January 17, 2017

CHAWATASO YALIA NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA YAITAKA SERIKALI KUDHIBITI WANAOCHOMA MISITU

Na Mwandishi wetu,    
Songea.

CHAMA cha Waganga wa jadi, wakunga na mangariba wa tiba asilia mkoani Ruvuma (CHAWATASO) kimetoa rai kwa serikali kuweka sheria kali itakayoweza kuwadhibiti watu wanaochoma misitu na kukata miti hovyo.

Mwenyekiti wa chama hicho, Mustafa Kafimbo amesema kuwa endapo hatua zisipochukuliwa za kudhibiti vitendo hivyo vya uharibifu wa misitu hali hiyo itasababisha miti mingi iliyokuwa ikitumika kutengenezea dawa kupotea na kuwa kero katika jamii.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti huyo wa CHAWATASO alipokuwa akizungumza kwenye mkutano wao uliofanyika mjini hapa huku akiongeza kuwa dawa nyingi ambazo hutumika katika jamii, zinatokana na majani ya miti asilia na mizizi hivyo vitendo vya ukataji wa miti na kuchoma misitu havipaswi kuendelea kufumbiwa macho.

Kafimbo ameiomba pia serikali kukitambua chama chao ambacho kilisajiliwa mwaka 2008 na kupewa namba ya usajili 17NGO/0441 kikiwa na jumla ya wanachama waanzilishi 13 mkoani hapa ambapo hivi sasa chama hicho kina wanachama 348.


Mwenyekiti huyo alisema kuwa kutokana na kuongezeka kwa vitendo vya uharibifu wa mazingira, kinaiomba serikali kukipatia chama hicho pia ardhi kwa ajili ya kupanda miti ili kukabiliana na tatizo la upungufu wa mvua ambalo linatokana na uharibifu wa mazingira.

Kwa upande wake Katibu wa CHAWATASO mkoani Ruvuma, Mayasa Mfaume naye alieleza kuwa chama hicho kimeendelea kutoa huduma ya tiba asilia kwa umakini mkubwa na kwamba kimekuwa pia kikipambana na kupinga vitendo vya uchawi na ramli chonganishi.

Mayasa amezitaja changamoto zinazowakabili kuwa ni baadhi ya vyama vya tiba asilia kujiona ni bora zaidi na kuanza vitendo vya kuwanyanyasa baadhi ya wanachama wa chama hicho kwa kuwanyang’anya tiba zao na kutozwa michango ambayo haitambuliki.

Katika kukabiliana na hali hiyo alishauri pawepo na shirikisho la umoja wa waganga wa tiba asilia ili kuweza kujenga sauti moja katika utoaji wa huduma bora za tiba asilia katika jamii na taifa kwa ujumla. 

Kadhalika mgeni rasmi katika mkutano huo Mbunge wa Songea mjini, Leonidas Gama ambaye aliwakilishwa na Katibu wake Kassian Mbawala alikipongeza CHAWATASO kwa kufanya kazi kwa maadili hali ambayo imechangia kuondokana na mila potofu za vitendo vya mauaji ya albino na kuendelea chama hicho kuwa kioo cha waganga wa jadi hapa nchini.

“Jamii inawategemea CHAWATASO katika masuala ya kujenga afya zetu kwa kutumia tiba mbadala, naomba endeleeni kuwa mabalozi wa kuhamasisha mila na desturi kwa kuwa katika kipindi hiki cha utandawazi vijana wengi wanadharau utamaduni wetu na kuiga utamaduni wa kigeni’’, alisema Mbawala.


Hata hivyo katibu huyo wa Mbunge wa Songea mjini ameahidi kutafutia ufumbuzi matatizo yote yanayoikabili chama hicho yakiwemo ya kunyanyaswa kwa baadhi ya wanachama wake ili yaweze kupatiwa ufumbuzi wa kudumu na hatimaye waweze kufanyakazi kwa amani na utulivu.

No comments: