Monday, January 2, 2017

TAMASHA LA UZINDUZI VIVUTIO VYA UTALII NYASA LAFANA WADAU WASHAURIWA KUWEKEZA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge akizungumza na wananchi, watendaji wa serikali na wageni kutoka nje ya mkoa huo (hawapo pichani) walipofika kwenye uzinduzi wa tamasha la kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo katika wilaya ya Nyasa mkoani hapa, upande wa kulia ni Mkuu wa wilaya hiyo Esabela Chilumba na kushoto Mbunge wa Jimbo la Nyasa, Stella Manyanya ambaye pia ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Injinia Stella Manyanya.
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge katikati akikata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa tamasha la kutangaza vivutio vya utalii katika wilaya ya Nyasa mkoani humo, upande wa kulia Mkuu wa wilaya ya Mbinga Cosmas Nshenye wa pili yake ni Mkuu wa wilaya ya Nyasa, Esabela Chilumba na kushoto ni Mbunge wa jimbo la Nyasa, Injinia Stella Manyanya.
Na Kassian Nyandindi,         
Nyasa.

TIMU ya viongozi wa serikali mkoa wa Ruvuma imewasili wilaya ya Nyasa mkoani humo kwa lengo la kushiriki tamasha la uzinduzi wa fursa za utalii huku serikali ikiwataka wadau kutoka maeneo mbalimbali ya ndani na nje ya mkoa huo kuwekeza wilayani humo kwenye shughuli za uvuvi, ujenzi wa hoteli za kisasa pamoja na viwanda vidogo vidogo.

Aidha imeelezwa kuwa ujenzi wa viwanda hivyo utasaidia kuifanya wilaya hiyo ipige haraka hatua mbele za kimaendeleo katika kuongeza thamani ya mazao yanayozalishwa, kukuza uchumi na kuleta ajira kwa vijana.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge alisema hayo juzi alipokuwa mgeni rasmi kwenye tamasha la uzinduzi wa fursa za utalii na kuinua uchumi wilayani Nyasa lililofanyika katika kituo cha udhibiti wa rasilimali za uvuvi wilayani humo.


Vilevile tamasha hilo lilishirikisha viongozi hao wa ngazi mbalimbali kwa lengo la kutangaza fursa za utalii zilizopo wilayani humo, ikiwemo fukwe za ziwa Nyasa samaki wa mapambo wenye rangi za aina mbalimbali, mazoezi ya kuogelea, visiwa vilivyopo ndani ya ziwa hilo, milima, mawe yenye kuvutia, shughuli za uvuvi na historia ya mambo ya kale.

Dkt. Mahenge aliwapongeza viongozi wa wilaya hiyo kwa kazi wanazozifanya katika kupigania maendeleo ya wananchi ambapo alisisitiza kwa kuwataka jitihada hizo ziendelezwe kwa kuwa wabunifu zaidi na kwamba serikali itaendelea kuunga mkono kwa ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo barabara.

Alifafanua kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2017 kuelekea 2018 serikali kuanzia mwezi Februari mwaka huu, itaanza kujenga barabara ya kutoka Mbinga mjini hadi Mbamba bay wilayani Nyasa kwa kiwango cha lami.

“Sisi kama serikali tutahakikisha tunafungua fursa hizi muhimu kwa kujenga barabara zilizokuwa katika viwango bora na tayari tumetangaza kujenga barabara hii kwa kiwango bora cha lami hivyo ili utalii uweze kutuletea mapato katika wilaya yetu ni lazima tuanze sasa kuwekeza kwanza sisi wenyewe”, alisisitiza Dkt. Mahenge.

Pia aliongeza kuwa fursa zinapokuja wananchi wanapaswa kufanya kazi kwa bidii kwa kuwa wepesi kushiriki shughuli mbalimbali za kimaendeleo kama vile kilimo cha mazao ya chakula na biashara ambayo yataweza kuwaletea kipato.

Hata hivyo tamasha hilo la uzinduzi wa fursa za utalii wilayani Nyasa ni endelevu na kwamba litakuwa likiadhimishwa kila mwaka ifikapo Disemba 30 kwa lengo la kutangaza na kukuza fursa za kiuchumi wilayani hapa, ikiwemo masuala ya utalii wa ndani ambao wananyasa wenyewe wanalojukumu kubwa la kuuimarisha ili uweze kuwa endelevu na kuwaletea kipato kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.




No comments: