Sunday, January 15, 2017

HALMASHAURI MAFIA YAJIWEKEA MIKAKATI YA KUONGEZA UZALISHAJI WA MAZAO



Na Julius Konala,  
Mafia.

HALMASHAURI ya wilaya ya Mafia mkoani Pwani, imejiwekea mikakati mbalimbali ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya biashara wilayani humo kutoka zao moja la nazi linalozalishwa sasa, hadi kufikia matatu ikiwemo zao la korosho kwa lengo la kuinua pato la halmashauri hiyo.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Erick Mapunda alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na gazeti hili ofisini kwake wilayani Mafia kwa lengo la kuelezea shughuli mbalimbali za maendeleo zinazofanywa na halmashauri hiyo.

Aidha Mapunda alisema kuwa mpaka sasa tayari wamekwisha tenga kiasi cha fedha kwa ajili ya kununulia kilo 200 za mbegu ya korosho, ambapo zitaweza kuzalisha  miche 1000 ambayo itagawiwa bure kwa wananchi na taasisi za shule.


Vilevile alisema halmashauri yake pia ina mpango wa kuzalisha zao la mbaazi ambalo litasaidia kuchangia kwa kiasi kikubwa kuinua pato la halmashauri pamoja na uchumi wa mtu mmoja mmoja katika wilaya hiyo.

“Ndugu mwandishi wa habari ninachotaka kukueleza hapa ni kwamba halmashauri yetu imekuwa nyuma kimapato kutokana na kutegemea makusanyo yake ya ushuru kwenye zao moja tu la biashara ambalo ni nazi za asili ambazo huzalishwa tani 35,000 kwa mwaka, pamoja na uvuvi ambapo makusanyo yake ni madogo jambo ambalo linatufanya tushindwe kutekeleza baadhi ya miradi ya maendeleo ya wananchi kutokana na kukosa vyanzo vingine vya mapato”, alisema Mapunda.

Katika kukabiliana na hali hiyo alisema kuwa halmashauri ina mpango wa kutoa elimu kwa wananchi juu ya upandaji miti mipya ya mikorosho, mbaazi pamoja na upimaji wa viwanja na walengwa kupewa hati miliki kwa lengo la kuinua pato la halmashauri, kukuza uchumi wa wananchi na kuondoa makazi holela

Pamoja na mambo mengine alizitaja changamoto anazokumbana nazo kuwa ni wananchi kutoshiriki kikamilifu kwenye shughuli za maendeleo hususani katika suala la upandaji wa miti mipya ya mikorosho na badala yake wamekuwa waking’ang’ania ile ya zamani ambayo haiwaletei tija.

No comments: