Monday, January 30, 2017

MBINGA WAPIGWA MARUFUKU KUWACHANGISHA FEDHA WANANCHI UJENZI VYUMBA VIPYA VYA MAABARA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge akizungumza na wananchi katika mikutano yake mbalimbali ya kusisitiza maendeleo mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,   
Mbinga.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge amewapiga marufuku viongozi wa wilaya ya Mbinga mkoani humo kuendelea kuwachangisha fedha wananchi wa wilaya hiyo kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vipya vya maabara na majengo mengine ya madarasa, hadi pale watakapokamilisha kuweka vifaa vinavyohitajika kwa majengo yaliyokuwa tayari.

DKt. Mahenge amelazimika kutoa ufafanuzi huo baada ya kupokea malalamiko hayo kutoka kwa wakazi wa Mbinga mjini, wakieleza kuwa wamekamilisha ujenzi wa vyumba vya maabara lakini bado havijaanza kutumika kwa kuwa serikali kupitia halmashauri ya mji huo haijapeleka vifaa hivyo kwa ajili ya matumizi ya wanafunzi.

Wakazi hao wa mji wa Mbinga walimuomba Dkt. Mahenge kutoa ufafanuzi juu ya michango hiyo inayoendelea kuchangishwa na Watendaji wa mitaa na kata, ambao wanawalazimisha wananchi kuendelea kutoa fedha licha ya kukamilika kwa vyumba vya maabara katika maeneo mbalimbali.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa mkoa alieleza kuwa sio busara kwa Watendaji hao kuendelea kuchangisha fedha wananchim, kwani  kila shule ya sekondari  ya serikali kuna maabara na sasa kilichobaki ni halmashauri kuhakikisha zinapeleka vifaa husika ili  maabara hizo ziweze kuanza kutumika.


Alisema kuwa agizo hilo pia linahusu hata katika miradi mingine  kama vile zahanati, vituo vya afya na hata katika maeneo mengine  ambako wananchi wameonekana kutekeleza wajibu wao na upande uliobaki ni wa serikali kupeleka vifaa, madaktari na dawa.

“Viongozi wenzangu lazima tuwe wa kweli, hakuna sababu ya kuendelea kuwataka wananchi wachangie fedha kwa ajili ya ujenzi wa maabara wakati zilizopo bado hazijaanza kutumika sasa nawashauri Wakurugenzi wa halmashauri za wilaya katika mkoa wetu Ruvuma, kuhakikisha mnapeleka vifaa husika ili maabara hizi zianze kutumika”, alisema Dkt. Mahenge.

Alisema kuwa lengo la serikali kujenga maabara hizo ni kuwajengea uwezo watoto waliopo shuleni waweze kusoma masomo ya sayansi, huku akisisitiza kuwa hakuna ulazima wa kuanza ujenzi mwingine wa majengo hayo hadi pale halmashauri hizo zitakapokamilisha zoezi la upelekaji vifaa.

Alifafanua kuwa endapo itaonekana kuna maeneo ambayo bado kazi ya ujenzi huo haijakamilika ndipo wananchi wanapaswa kushirikishwa kutoa michango yao badala ya kuwachosha kwa kuwachangisha michango mingi isiyokuwa ya lazima.

Dkt. Mahenge aliongeza kuwa kinachofanywa na serikali hivi sasa ni kukamilisha maabara hizo kwa kuzipatia vifaa vyote, ili watoto waweze kupata fursa ya kupata maarifa ambayo yatakuwa na manufaa makubwa kwa taifa.

Pia alibainisha kuwa kwa kutambua umuhimu wa wataalamu wa masomo ya sayansi serikali itaendelea kutenga fedha mwaka hadi mwaka, ili kujenga na kuboresha miundombinu ya shule, afya, maji na bara bara hatua ambayo itasaidia kuharakisha ukuaji wa uchumi katika  mkoa huo.

Alisema kuwa lengo ni kutaka kuona elimu inayotolewa inaendana na mahitaji halisi katika ulimwengu wa sasa wa sayansi na teknolojia, unaohitaji wataalamu wenye maarifa na uelewa wa kutosha katika fani mbalimbali pamoja na watu wenye afya njema na miundombinu bora.

No comments: