Monday, January 9, 2017

SERIKALI KUICHUKULIA HATUA KAMPUNI YA TANCOAL ENERGY

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiagana na Mkuu wa mafunzo na utendaji kivita wa brigedi ya Tembo Songea mkoani Ruvuma, Kanali Samwel Makabala katika uwanja wa ndege wa Songea jana mara baada ya Waziri Mkuu kuhitimisha ziara yake ya kikazi ya siku nne mkoani hapa.
Na Kassian Nyandindi,         
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameitaka kampuni inayojishughulisha na uchimbaji wa madini ya makaa ya mawe Tancoal Energy, kwenye mgodi wa Ngaka wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kutekeleza makubaliano ambayo yapo kwenye mikataba kabla serikali haijachukua hatua zaidi.

Agizo hilo lilitolewa na Waziri Mkuu Majaliwa jana alipokuwa akizungumza na viongozi mbalimbali wa mkoa huo kwenye kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku nne ya kikazi mkoani hapa, ya kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo ambapo alisisitiza kuwa endapo kampuni hiyo haitatekeleza makubaliano husika ya mikataba iliyoingia na serikali, italazimika kuizuia isiendelee na kazi ya uchimbaji wa makaa hayo na kuitafuta kampuni nyingine ambayo itaridhia makubaliano ambayo yataleta manufaa kwa Watanzania juu ya uendeshaji wa mgodi huo.

“Nilipata fursa ya kukagua shughuli mbalimbali za mgodi wa makaa ya mawe wa Ngaka nimejionea mwenyewe shughuli za uchimbaji wa makaa haya na uzalishaji wa umeme unaotekelezwa na kampuni ya Tancoal Energy, ambayo ni kampuni ya ubia kati ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) na kampuni ya Pacific Coparation East Africa ya Australia”, alisema Majaliwa.

Pia alieleza kuwa pamoja na kazi nzuri inayofanyika kwenye mgodi huo, amebaini kuwepo kwa mapungufu mengi yakiwemo Shirika hilo la maendeleo la taifa kutolipwa gawio lake (Dividend) tangu ulipoanza uzalishaji wa makaa hayo mwaka 2011.


Waziri Mkuu huyo alifafanua kuwa kampuni hiyo pia imeanza kuzalisha na uzalishaji huo unaendelea kuongezeka siku hadi siku, pia serikali imefanikiwa kuongeza masoko kwa kuzuia uingizaji wa makaa ya mawe kutoka nje ya nchi ambapo Tancoal Energy ya Ngaka wilayani Mbinga na Tanzacoal ya Kiwira wilayani Rungwe mkoa wa Mbeya, zinazotokana na kampuni moja ya Australia Intra Energy Corporation Limited (IEC) ndio wazalishaji wakubwa wa makaa hayo hapa nchini lakini kampuni ya Tancoal inaeleza kwamba inapata hasara kila mwaka jambo ambalo amedai kuwa sio la kweli.

“Kampuni inatuambia kila mwaka imekuwa inapata hasara jambo hili haliaminiki, serikali haitakubali kuona hali hii inaendelea nataka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) akague mahesabu yote ya kampuni hii ikibainika wanadanganya, Tancoal Energy watawajibika kulipa gawio la serikali tokea mgodi ulipoanza”, alisisitiza.

Vilevile amemtaka Mwanasheria mkuu wa serikali aone umuhimu wa kupitia upya mkataba baina ya kampuni hiyo ya mgodi wa makaa ya mawe na Shirika la maendeleo la taifa, ili kuuboresha na pia kuona uwezekano wa kuongeza hisa za NDC pia kama itashindikana washauri namna ya Tancoal Energy kujitoa katika mkataba huo.

Waziri Mkuu Majaliwa ameitaka pia Wizara ya viwanda na biashara isimamie kikamilifu utendaji wa NDC pamoja na kampuni ya Tancoal Energy ili kuhakikisha kuwa makubaliano yaliyofikiwa katika mkataba huo, yanatekelezwa ipasavyo na kwamba serikali ishauriwe namna ambavyo mapungufu yote yatakavyoondolewa.


Hata hivyo Waziri Mkuu huyo ameishushia lawama kampuni hiyo kuwa hadi sasa haijatekeleza makubaliano yaliyofikiwa na serikali katika mikataba husika ikiwemo ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, kutoka kijiji cha Kitai ambako kuna bandari kavu ya kupakia makaa ya mawe hadi mgodini yanakochimbwa makaa hayo, ujenzi wa mitambo ya ufuaji wa umeme na kuimarisha tekinolojia ya kuchimba makaa hayo ya mawe.

No comments: