Saturday, January 7, 2017

MKURUGENZI NDC AKALIA KUTI KAVU WAZIRI MKUU ABAINI MADUDU MGODI MAKAA YA MAWE MBINGA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiangalia makaa ya mawe katika mgodi wa Ngaka yanayochimbwa na kampuni ya Tancoal Energy, kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga jana alipotembelea mgodi huo kwa ajili ya kujiridhisha kama kamapuni hiyo inalipa kodi kwa serikali ipasavyo na kubaini kwamba tangu mwaka 2011 mgodi huo ulipoanza ulipaji wake wa kodi umekuwa ni tatizo.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

MKURUGENZI Mtendaji wa Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) Mlingi Mkucha amejikuta akiwa katika wakati mgumu baada ya kushindwa kutolea ufafanuzi mbele ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa juu ya kodi ya gawio la serikali inayopatikana katika mgodi wa makaa ya mawe Ngaka uliopo katika kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma.

Aidha kufuatia hali hiyo, serikali hapa nchini imesema kuwa itamtuma Gavana wake wa Benki kuu pamoja na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwenda kufuatilia mwenendo mzima wa fedha za kodi ya serikali katika mgodi huo, ili kuweza kujiridhisha kama kodi hiyo ilikuwa inalipwa serikalini ipasavyo au la.

Hayo yalijitokeza jana mbele ya Waziri Mkuu, Majaliwa alipokuwa katika ziara yake ya kikazi mkoani hapa, baada ya kutembelea mgodi huo kwa lengo la kujionea maendeleo yake na changamoto mbalimbali zilizopo ambapo alisema kuwa endapo ukweli ukibainika baada ya ukaguzi kufanyika, wahusika walioshiriki kukwepa kulipa kodi hiyo watawajibika kulipa tangu mgodi huo ulipoanza.


Waziri Mkuu Majaliwa alifafanua kuwa kuna harufu ya ufisadi juu ya fedha hizo za serikali ambapo tokea mgodi huo uanzishwe mwezi Julai mwaka 2011 serikali imekuwa haipati gawio lake la kodi ipasavyo, hivyo ameagiza ukaguzi ufanyike haraka ili kuweza kujiridhisha fedha hizo zilizokuwa zikipatikana kutokana na mauzo ya makaa ya mawe zilikuwa zikipelekwa wapi.

“Nimegundua nyie mmeamua kubana mianya ya serikali kupata fedha zake, kama hamtaweza kusimamia hili NDC tutamweka mtu ambaye atasimamia jambo hili ili serikali iweze kupata fedha zake, haiwezekani mnaendelea kuzalisha malighafi halafu serikali bado inapata hasara”, alisema.

Alisema kuwa mgodi wa Ngaka ni mgodi ambao unatoa makaa ya mawe yenye viwango vya ubora wa hali ya juu katika bara la Afrika, hivyo una kila sababu ya kuwanufaisha Watanzania wenyewe na sio vinginevyo.

Vilevile aliongeza kuwa atamtuma Mwanasheria mkuu wa serikali apitie mikataba yote ya mgodi huo kwani inaonesha kuna utata mkubwa ambao unaisababishia serikali kukosa fedha zake za gawio la kila mwaka la kodi itokanayo na mauzo ya makaa hayo na kusababisha iendelee kupata hasara.

Alisema kuwa serikali ya awamu ya tano imedhamiria kukusanya kodi kikamilifu sambamba na kupitia mikataba yote ya makampuni yanayojishughulisha na uchimbaji wa madini hapa nchini, ili kuona namna gani nchi inanufaika na rasilimali zake.

Majaliwa aliongeza kuwa ni vyema shirika la NDC likawa makini katika kuhakikisha kwamba linaisimamia ipasavyo kampuni ya TANCOAL Energy inayochimba makaa ya mawe katika mgodi wa Ngaka, uliopo kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma ikiwa ni pamoja na kulipa mapato ya serikali kama inavyotakiwa.

Katika hatua nyingine akizungumza na wananchi wa kata hiyo Waziri Mkuu huyo aliitaka kampuni hiyo kuhakikisha inatekeleza jukumu lake la kupeleka maji safi na salama katika maeneo wanaoishi wananchi waliopo karibu na mgodi, sambamba na kusaidia kuboresha miundombinu ya shule za msingi kama walivyokubaliana katika mikataba husika.

Vilevile alimuagiza Mbunge wa Jimbo la Mbinga vijijini, Martin Msuha kufuatilia masuala hayo yanayotakiwa kutekelezwa na kampuni hiyo kwa wananchi ili iweze kukamilika kwa wakati na kuondoa malalamiko yasiyokuwa ya lazima.


Alisisitiza pia juu ya umuhimu wa kampuni hiyo kujenga barabara ya kutoka Kitai hadi mgodini kwa kiwango cha lami, ili kuwaondolea adha wananchi kupata vumbi linatokana na makaa hayo wakati yanaposafirishwa kutoka mgodini kwenda kwa wateja.

No comments: