Sunday, January 8, 2017

MAJALIWA: VIONGOZI BODI YA KOROSHO WAKAMATWE

Na Kassian Nyandindi,         
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameuagiza uongozi wa serikali ya mkoa wa Mtwara kuwakamata mara moja viongozi wanne wa Bodi ya zao la korosho Tanzania, akiwemo Kaimu Meneja mkuu wa Chama cha ushirika wilaya ya Masasi (MAMCU) mkoani humo Kelvin Rajab baada ya kubaini kuwepo mapungufu makubwa ya wizi wa korosho za wakulima.

Aidha aliwataja viongozi wengine watatu ambao Waziri Mkuu huyo alisema kuwa wameshiriki kwa namna moja au nyingine kuhujumu korosho hizo za wakulima na wanapaswa kukamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya dola kuwa ni Lawrence Njozi ambaye ni Meneja wa tawi chama kikuu cha ushirika MAMCU, Yusuph Namkukula ambaye ni Mkurugenzi na Ramadhan Namakweto wa kampuni ya YURAP ambayo ilikuwa ikishiriki kwenye minada ya manunuzi ya zao hilo.

Majaliwa alitoa agizo hilo leo alipokuwa kwenye kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku nne ya kikazi mkoani Ruvuma, kwenye ukumbi wa mikutano Ikulu ndogo mjini Songea.


Alifafanua kuwa mapungufu mengine yaliyojitokeza kuhusiana na usimamizi wa mauzo ya korosho hizo kuwa ni wakulima katika wilaya ya Masasi, kulipwa kilo pungufu ya zile zilizowasilishwa kwenye maghala bila kupewa maelezo ya aina yoyote kinyume cha maagizo ya serikali.

Vilevile alieleza kuwa wakulima kutolipwa fedha za mauzo ya zao la korosho yaliyofanyika kwenye mnada wa tano Novemba 10 mwaka jana, bila kuwepo maelezo kamilifu licha ya kuwa chama kikuu cha ushirika cha MAMCU kilishauza zao hilo kwenye minada na malipo kufanyika.

Alieleza kuwa tani 2,138 za korosho katika maghala ya Mtandi na Buco kutopelekwa mnadani kwa makusudi tangu Novemba 11 mwaka jana, taarifa ya kuwepo au kutokuwepo korosho hizo kutokutolewa kwa mamlaka husika na kuwasababishia hasara kubwa wananchi na serikali kukosa mapato yake.

Kadhalika aliongeza viongozi hao kushindwa kufuatilia malipo ya zao hilo tani 1,156,262 ambazo ziliuzwa kwenye mnada wa kumi uliofanyika Disemba 21 mwaka jana ambapo korosho hizo zilinunuliwa na Maviga East Africa tani 503,297, Machinga Transport tani 104,200, Tastey tani 319,576 na Saweya Impex tani 229,189.  

Pamoja na mambo mengine, Waziri Mkuu Majaliwa aliipongeza bodi mpya ya korosho kwa kusimamia kikamilifu minada iliyofanyika ya zao hilo na kuweza kubaini mapungufu yaliyojitokeza na izingatie maelekezo ya serikali kuhakikisha kwamba wanunuzi wa zao hilo wanaweka dhamana ya fedha za ununuzi wa korosho kabla ya kuruhusiwa kununua.


Hata hivyo alisisitiza kwa kumtaka Mrajisi wa vyama vya ushirika mkoani Mtwara kuona umuhimu wa kuzingatia maagizo yanayotolewa na serikali ikiwa ni pamoja na kuziondoa changamoto za kuwalipa wakulima kwa bei za mnada wa chini ili waweze kuuza kwa bei za mnada wa juu na mkulima alipwe kwa bei ya mnada wake alipouza korosho na sio vinginevyo.

No comments: