Thursday, January 5, 2017

NFRA KANDA YA SONGEA YATAKIWA MAHINDI ILIYONUNUA KUYATUNZA VIZURI

Meneja wa wakala wa taifa wa hifadhi ya chakula NFRA Kanda ya Songea Majuto Chabuluma wa kwanza kushoto akimuonesha Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kiasi kidogo cha mahindi kilichonunuliwa na NFRA, ambayo msimu huu imeshindwa kufikia malengo ya  kununua tani 22,000 badala yake imenunua tani 10,335.256 tu, kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge.
Na Kassian Nyandindi,         
Songea.

WAKALA wa Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) Kanda ya Songea mkoani Ruvuma, ametakiwa kuhakikisha kwamba mahindi yote yaliyonunuliwa yanatunzwa vizuri kwa umakini mkubwa, hayaharibiki katika maghala ya kuhifadhia chakula ili yaweze kusaidia pale itakapotokea tatizo la njaa hapa nchini.

Agizo hilo limetolewa jana na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa alipokuwa ametembelea kituo cha hifadhi hiyo kilichopo katika Manispaa ya Songea mjini hapa.

“Hakikisheni mahindi haya yanatunzwa vizuri ili yasiweze kuharibika, yasije yakatokea kama msimu uliopita mwaka jana mahindi mengi yaliharibika hivyo serikali hatutaki kuona tena mwaka huu tatizo hili linajirudia”, alisisitiza Majaliwa.

Alifafanua kuwa serikali kupitia kitengo chake cha kuhifadhi chakula kila mwaka kipo kwa ajili ya kununua kiasi kidogo cha ziada ya chakula na sio vinginevyo, ikiwa ni lengo la kuweka tahadhari pale yanapotokea matatizo ya njaa.


“Serikali imekuwa ikitoa fedha nyingi mwaka hadi mwaka, kwa ajili ya kununua chakula hivyo ni wajibu wa wafanya kazi wa idara hii kukitunza ili kisiweze kuharibika kwa ajili ya matumizi ya baadaye”, alisema.

Kadhalika alieleza kuwa endapo kuna kiongozi yeyote wa serikali ana wasiwasi juu ya hali iliyopo katika msimu wa mwaka huu, kutokana na mvua kuchelewa kunyesha na hali ya joto kali tofauti na misimu mingine ni muhimu kuwahimiza wananchi wajiwekee akiba ya chakula ili kiweze kuwasaidia katika familia zao.

NFRA Kanda ya Songea imepongezwa pia kwa juhudi kubwa inazofanya ya ununuaji wa mahindi, pamoja na kwamba haikutimiza lengo la serikali kutokana na ushindani mkubwa wa kibiashara kutoka kwa watu binafsi.

Awali Meneja wa Wakala huyo wa hifadhi chakula Kanda ya Songea, Majuto Chabuluma alimweleza Waziri Mkuu kwamba, serikali  katika bajeti yake ya mwaka wa fedha wa 2016/2017 iliidhinisha kwa wakala wa taifa wa hifadhi ya chakula kununua jumla  ya tani 100,000 za mahindi kwa nchi nzima.

Kwa kanda ya Songea mkoani Ruvuma ilipangiwa kununua tani 22,000 kutoka kwa wakulima katika maeneo ya vijijini ambapo kazi ya ununuzi huo ilianza Aprili 22 mwaka jana baada ya kukamilisha ufunguzi wa vituo 26 vya ununuzi wa mahindi.

Majuto alieleza kuwa vituo hivyo vilifunguliwa katika maeneo ya vijijini kwa lengo la kutekeleza maagizo ya serikali ya kuhakikisha kwamba, wakala anawafikia wakulima wa mahindi kwa bei nzuri inayotolewa na serikali.

Hadi kufikia Disemba 27 mwaka jana Kanda ya Songea ilikuwa imekwisha nunua tani 10,335,256 za mahindi kati ya tani 22,000 ambazo zilipangwa kununuliwa na kwamba changamoto kubwa iliyojitokeza kwenye zoezi la ununuzi wa msimu huo ni mwenendo usioridhisha wa wakulima katika kupeleka mazao yao kwenye vituo vya ununuzi vya NFRA ambapo mengi walikuwa wakiyauza kwa wafanyabiashara binafsi hivyo kufanya wakala huyo kushindwa kufikia malengo husika.

Aidha Majuto alisema kuwa sababu nyingine iliyochangia hilo ni kuchelewa kuanza kwa zoezi la ununuzi ambapo kawaida msimu wa ununuzi hufunguliwa baada ya mwaka wa fedha wa serikali, yaani mwezi Julai ambapo hazina hutuma fedha kwa wakala kwa ajili ya kutekeleza kazi hiyo baada ya vikao vyao vya bajeti kumaliza kuketi.

Katika msimu wa mwaka huu maeneo mengi mkoani Ruvuma yanakabiliwa na upungufu wa chakula hivyo wanunuzi wengi binafsi waliwahi kwenda huko kwa wakulima, kununua mahindi na kuyahifadhi katika maghala yao ikizingatiwa kwamba mkoa huo ni tegemeo kubwa la kutoa chakula cha ziada kwa maeneo mengine hapa nchini.

Hata hivyo sababu nyingine iliyojitokeza ya kushindwa kufikia malengo alisema kuwa ni pamoja na ushindani wa bei ambapo bei iliyotolewa na wanunuzi binafsi ilikuwa juu tofauti na ile iliyotolewa na serikalia kwa NFRA.


No comments: