Sunday, February 4, 2018

MENEJA TRA MKOA WA MARA ASIMAMISHWA KAZI


Na Mwandishi wetu,

KAMISHNA Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Kichere amemsimamisha kazi Meneja wa Mamlaka hiyo Mkoa wa Mara, Nicodemus Mwakilembe kutokana na uzembe wa kutosimamia ipasavyo matumizi ya Mashine za Kielektroniki (EFDs) ambazo hutumika kutolea risiti kwa wafanyabiashara wa Mkoani humo.

Hatua hiyo ya kusimamishwa kazi imetokana na ziara ya kushtukiza iliyofanywa ya kukagua matumizi ya Mashine hizo aliyoifanya Kamshina huyo kwenye baadhi ya maduka ya biashara Wilayani Bunda Mkoa wa Mara.

Akizungumza mara baada ya ziara yake, Kichere alisema kuwa Meneja huyo ameonyesha uzembe wa hali ya juu kwani kuna wafanyabishara wengi Mkoani kwake, ambao walikwisha lipa fedha kwa ajili ya kupata mashine za EFDs lakini mpaka sasa hawajapatiwa mashine hizo.


“Katika ziara yangu nimegundua kwamba wapo wafanyabiashara ambao walikwisha lipia mashine hizi miaka kadhaa iliyopita lakini mpaka sasa, bado hawajapatiwa mashine zao na wamekuwa wakitumia mwanya huo kama kinga ya kutochukuliwa adhabu na TRA wakati Meneja wa Mkoa yupo na hachukui hatua yoyote, huu ni uzembe uliopitiliza na kamwe siwezi kuuvumilia”, alisisitiza Kichere.

Kutokana na uzembe huo, Kamishna huyo amewaagiza Mameneja wote wa TRA hapa nchini pamoja na majukumu mengine kuhakikisha wanasimamia kikamilifu matumizi ya mashine za EFDs katika mikoa yao na kuongeza kuwa hatasita kumwajibisha Meneja yeyote atakayeshindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

No comments: