Tuesday, February 13, 2018

SERIKALI YABAINI NJIA ZINAZOTUMIKA KUPITISHA DAWA ZA KULEVYA

Upande wa kushoto ni Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikabidhi gari kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Rogers Sianga katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi wetu,

KASSIM Majaliwa ambaye ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amesema kuwa Serikali imebaini kwamba maeneo ya bahari kuu, bandari, vituo vya mabasi pamoja na viwanja vya ndege hapa nchini ndiyo yanatumika zaidi kupitisha dawa za kulevya.

Wafanyabiashara, wasambazaji na watumiaji wa dawa hizo alisema kuwa wamekuwa wakikamatwa lengo ikiwa ni kuhakikisha kwamba biashara hiyo inakomeshwa na kumalizika kabisa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Ofisi ya Waziri Mkuu imesema kuwa Waziri huyo ametoa kauli hiyo wakati akikabidhi gari kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Rogers Sianga katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.


Alieleza kuwa mbali na kukamata meli pia Serikali imewakamata wasambazaji pamoja na kundi kubwa la wafanyabiashara wanaojihusisha na biashara hiyo sambamba na watumiaji.

Majaliwa alifafanua kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha Tanzania inakuwa salama na kizazi chenye uwezo wa kuzalisha mali.

Aliongeza kuwa Serikali imepiga hatua kubwa katika vita dhidi ya dawa za kulevya na kwamba hivi karibuni imeweza kukamata meli nyingi, moja ikiwa inatokea pwani ya Msumbiji na ilikamatiwa maeneo ya Mtwara ikiwa na dawa nyingi za kulevya.

“Ni wakati wa Serikali sasa kuendelea kuiwezesha Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya na leo hii tunawakabidhi gari hili jipya kabisa ili liweze kuendelea na utekelezaji wa majukumu yake ipasavyo”, alisema.

Kadhalika amewataka Watanzania waachane na biashara ya dawa za kulevya ikiwa ni pamoja na kazi ya kusambaza, kuzalisha, kutumia na wale watakaokamatwa wakijihusisha nazo watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Alisema hivi sasa Serikali inajenga maabara ambayo itatumiwa na Mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa dawa wanazozikamata.

Wananchi wanatakiwa kushirikiana na Serikali katika vita dhidi ya dawa za kulevya kwa kutoa taarifa mara wanapowabaini wafanyabiashara, watumiaji na wasambazaji wa dawa hizo.

Pia wahakikishe wanawalinda vijana ili wasijihusishe na dawa za kulevya.

Kwa upande wake, Sianga ameishukuru Serikali kwa kuipatia mamlaka hiyo gari ambapo alitumia fursa hiyo kuwataka wananchi waachane na biashara hiyo huku akiwasihi kupambana kuhakikisha dawa za kulevya haziingizwi nchini.

Hata hivyo mbali na kudhibiti biashara hiyo alisema pia wanatoa elimu juu ya madhara ya matumizi ya dawa za kulevya, ikiwemo vitendo viovu vinavyofanywa na watumiaji ili wachukie na waache kutumia dawa hizo.

No comments: