Wednesday, February 21, 2018

SERIKALI YATAKIWA KUONGEZA KIASI CHA FEDHA UJENZI WA BARABARA TUNDURU


Na Kassian Nyandindi,   
Tunduru.

KATIKA kuchochea kasi ya ukuaji wa maendeleo katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma, Serikali imeombwa kuongeza fedha kwa ajili ya ujenzi na uimarishaji wa miundombinu ya barabara hasa vijijini Wilayani humo, ambazo hazifanyiwa matengenezo kwa muda mrefu.

Imeelezwa kuwa endapo litatekelezwa hilo hata shughuli za kiuchumi ambazo zinazofanywa na wananchi wataweza kutekeleza kwa urahisi na hatimaye Wilaya nayo kuweza kunufaika na kupiga hatua katika ukuaji wa mapato yake.

Hivi sasa kiasi cha fedha kinachotolewa na Serikali kwa ajili ya ujenzi wa barabara hizo imeelezwa kuwa ni kidogo ikilinganishwa na mahitaji halisi yanayotakiwa, kwa kuwa Wilaya hiyo ni kubwa na imekuwa na mtandao mkubwa wa miundombinu ya barabara wenye urefu wa Kilometa 1,261.2 sawa na Mkoa jirani wa Mtwara.


Ombi hilo limetolewa jana na Meneja wa Wakala wa Barabara Mjini na Vijijini (TARURA) Wilayani Tunduru, Mhandisi Cyprian Kimwaga alipokuwa akizungumzia kuhusiana na ubovu wa barabara hizo katika Wilaya hiyo.

Kimwaga alifafanua kuwa Wilaya ina jumla ya barabara ambazo zipo kwenye mtandao wa Wakala huyo ni 216 na kwamba kati ya hizo barabara za lami ni Kilometa 1.371, changarawe Kilometa 81.388, udongo Kilometa 1178.44 ambapo kati ya hizo zinazopitika kipindi chote cha mwaka ni barabara zenye Kilometa 400 tu.

Alisema kuwa katika msimu wa mwaka huu 2018/2019 TARURA Wilayani humo wamejipanga kuhakikisha kwamba wanajenga madaraja, vivuko na makalvati ili barabara hizo ziweze kupitika kabla ya kuendelea na ujenzi husika.

Pia alieleza kuwa mkakati mkubwa walionao sasa ni kutoka katika ujenzi wa barabara za changarawe hadi kufikia kiwango cha lami na kwamba hivi sasa wanakamilisha, ujenzi wa barabara ya Milonde hadi Kalulu yenye urefu wa Kilometa 26 ambayo ilikuwa katika hali mbaya kipindi hiki cha masika ambapo wananchi wamekuwa wakishindwa kutumia barabara hiyo na hakuna magari yaliyoweza kufika kwenye maeneo hayo kutoa huduma ya usafiri.

“Kutokana na hali hii wananchi wanalazimika kutembea kwa miguu au Pikipiki kwa gharama kubwa katoka sehemu moja kwenda nyingine barabara hii ni muhimu sana kiuchumi kwa Wilaya ya Tunduru kwani ndiyo eneo lenye uzalishaji mkubwa wa mazao mchanganyiko,

“Kazi iliyofanyika katika barabara ile ni kupunguza milima, kuweka changarawe katika maeneo yaliyokuwa na utelezi vilevile tutaendelea kufanya hivyo hata katika barabara za udongo ambazo zinakwenda katika maeneo yenye uzalishaji mkubwa”, alisema Kimwaga.

Aliongeza kuwa barabara nyingine ambayo wanatarajia kuanza ujenzi wake ni ile inayoanzia Kalulu hadi kwenye hifadhi ya Selou yenye urefu wa Kilometa 40 ambayo nayo ni muhimu kwa kukuza uchumi wa Wilaya na kurahisisha kuleta Watalii waweze kupita vizuri bila vikwazo au usumbufu wowote ule.

No comments: