Tuesday, February 6, 2018

USIMAMIZI UJENZI WA KITUO CHA AFYA KALEMBO UNAENDELEA VIZURI

Baadhi ya viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mbinga na watendaji wa Halmashauri ya Mji wa Mbinga, wakiwa katika picha ya pamoja katika eneo la ujenzi wa Kituo cha afya Kalembo kilichopo katika kata ya Kihungu kwenye Halmashauri hiyo ambapo walitembelea juzi katika eneo hilo kwa ajili ya kujionea maendeleo ya ujenzi wake.


Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

UJENZI wa Kituo cha afya Kalembo katika kata ya Kihungu Halmashauri Mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma, imeelezwa kuwa unaendelea vizuri na umefikia katika hatua ya mwisho kukamilisha baadhi ya vipengele vya ujenzi wa majengo husika.

Hayo yalisemwa juzi na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilayani humo, Beda Hyera mara baada ya kutembelea Kituo hicho na kujionea uhalisia wa kazi zinazofanyika.

Hyera alisema kuwa ujenzi huo ambao unafanyika na usimamizi wake ameridhishwa nao kwamba unaendelea vizuri.


Amewapongeza Mwenyekiti Kipwele Ndunguru na Mkurugenzi wake wa Halmashauri ya Mji huo, Robert Kadaso Mageni kwamba waendeleze jitihada hizo za kukamilisha kazi ya ujenzi huo ili wananchi wa kata ya Kihungu waweze kupata huduma ya matibabu kwa urahisi.

Vilevile alieleza kuwa Serikali ya CCM inayoongozwa na Dokta John Pombe Magufuli, haitaki kuona wananchi wake wanapata shida ndiyo maana imetengeneza Ilani ya chama hicho ambayo inatetea maslahi ya mwananchi hivyo hata viongozi waliowekwa madarakani, wanapaswa kusimamia kikamilifu miradi inayotekelezwa na Serikali hiyo ili kuweza kuondoa kero zinazoikabili jamii.

“Ndugu zangu Serikali hii malengo yake ni kuhakikisha kwamba wananchi wake wanapata haki sawa katika nyanja ya elimu, afya miundombinu ya barabara na mambo mengine muhimu yote ambayo Mtanzania anapaswa kuyapata”, alisema Hyera.

Hata hivyo Serikali kwa ujumla, imetoa fedha zaidi ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo hicho cha afya Kalembo kilichopo katika kata ya Kihungu Halmashauri ya Mji wa Mbinga kwa ajili ya kufanya kazi ya kukamilisha ujenzi wa jengo la upasuaji, maabara, wodi ya akina mama na watoto, nyumba ya mganga pamoja na jengo la kuhifadhia maiti.

No comments: