Tuesday, February 20, 2018

WAZIRI JENISTA MHAGAMA ATAKA WAWEKEZAJI KUTHAMINIWA


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira na Walemavu ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Peramiho Wilayani Songea Jenista Mhagama akiangalia sehemu ya makaa ya mawe yaliyochimbwa na Kampuni ya Kambas Group of Companies katika kijiji cha Maniamba kata ya Muhukuru Halmashauri ya Wilaya hiyo, upande wa kulia kwake ni Mwenyekiti wa Kampuni hiyo Yahaya Yusuphu na wa kwanza kulia ni Mhandisi wa madini wa Kampuni, Timoth Malima.


Na Muhidin Amri,        
Songea.

JENISTA Mhagama ambaye ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge, Ajira na Watu wenye ulemavu ameitaka Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma kuhakikisha wanatumia vizuri asilimia tatu ya mapato yatokanayo na shughuli zitakazoanza za uchimbaji wa makaa ya mawe katika kijiji cha Maniamba kata ya Muhukuru Wilayani humo.

Aidha amesema wanapaswa kuweka mazingira bora yatakayoweza kuwavutia wawekezaji, ambapo hatua hiyo itaweza kutoa fursa kwa wawekezaji wengi kuweza kuwekeza ili mradi huo wa makaa ya mawe uweze kusonga mbele.

Hivi sasa Kampuni ya Kambas Group of Companies imeweza kuanza kuwekeza katika kijiji hicho ili kuweza kufanya kazi zake katika mazingira rafiki ya uchimbaji wa makaa hayo, hivyo Halmashauri hiyo ameitaka pia kuweka mazingira mazuri ambayo hawataweza kukimbiwa na wawekezaji hao.


Waziri Mhagama ametoa agizo hilo jana, huku akiwaonya pia viongozi wa kijiji cha Maniamba akiwataka kuwa waaminifu wa fedha kwa kujiepusha na tabia ya wizi na kuwataka kutumia mapato hayo, kwa ajili ya kusomesha vijana wao wa kijiji hicho ili wapate ujuzi utakaowawezesha kuwa na sifa nzuri ya kufanya kazi kwenye mgodi huo.

Hayo yalisemwa na Waziri huyo alipokuwa akizungumza na wakazi wa kijiji hicho, Wakuu wa idara ya Halmashauri ya Wilaya hiyo wakati alipotembea katika eneo hilo ili kuweza kujionea kazi ya utafiti wa makaa ya mawe inayoendelea kufanyika katika kijiji cha Maniamba na Kampuni ya Kambas Group of Companies.

Alisema kuwa Serikali ya awamu ya tano imejipanga kuhakikisha kwamba nchi ya Tanzania inafikia uchumi wa kati kwa kuanzisha viwanda vingi ambavyo vitasaidia kukua kwa uchumi wake na Watanzania wengi waweze kupata ajira katika viwanda hivyo.

Mhagama ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Peramiho alieleza kuwa hivi sasa Watanzania wapatao milioni 25 ndiyo wenye uwezo wa kufanya kazi na kwamba kati yao asilimia 56 ni vijana ambao wapo katika ajira isiyokuwa rasmi na ile ajira rasmi.

Alifafanua kuwa kutokana na kuwepo kwa tatizo hilo Serikali imehamasisha na itaendelea kuhamasisha shughuli za uwekezaji ili watu wake waweze kupata ajira hasa kwa wale wazawa na hatimaye kukuza uchumi wa nchi yetu.

Vilevile ameipongeza Kampuni hiyo kwa hatua iliyochukua ya uamuzi wake wa kuwekeza katika utafutaji na uchimbaji wa makaa ya mawe katika jimbo la Peramiho.

Hata hivyo amewataka wamiliki wa Kampuni ya Kambas Group of Companies kufuata sheria zilizowekwa ikiwemo utoaji wa mapato ya asilimia 0.3 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Songea, ushuru wa kijiji cha Maniamba na kuzingatia maslahi kwa wafanyakazi wake ili kuepuka migogoro inayoweza kusababisha kazi ya uchimbaji wa madini hayo kukwama.

No comments: