Sunday, December 13, 2015

HALMASHAURI ZA WILAYA RUVUMA ZATAKIWA KUPELEKA ASILIMIA 10 KWA WANAWAKE NA VIJANA



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MBUNGE wa Viti maalum mkoani Ruvuma, Jacqueline Msongozi amezitaka Halmashauri za wilaya mkoani humo kutekeleza jukumu la kupeleka asilimia 10 ya fedha za mapato yake ya ndani katika vikundi vya ujasiriamali, kwa wanawake na vijana.

Aidha amewaagiza madiwani wa mkoa huo, kuhakikisha kwamba suala hilo wanalifuatilia kwa karibu ndani ya Halmashauri zao kupitia vikao husika, ili fedha hizo zielekezwe kwa kundi hilo.

Msongozi alitoa agizo hilo, alipokuwa akizungumza na akina mama wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) tawi la Mbinga, katika kikao cha baraza la wanawake kilichofanyika kwenye ukumbi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) uliopo mjini hapa.


Mbunge huyo alisema kuwa wanawake wanaweza kujituma kwa kila jambo la kimaendeleo, hivyo wanapaswa wakati wote kutetea haki zao pale wanapoona zinaporwa na watu wasiopenda maendeleo yao.

“Madiwani mliochaguliwa nawataka pia mrudi kwenye kata zenu kutumikia wananchi na sio muda mwingi kuwa mbali, tabia ya kutengeneza majungu na fitina tuache sasa tuunge mkono kauli mbiu ya Rais wetu John Magufuli, ‘Hapa kazi tu’ kwa kufanya kazi kwa ushirikiano kwa maendeleo ya taifa letu”, alisema Msongozi.

Vilevile aliwataka wanawake kujiunga katika vikundi vya ujasiriamali, ili waweze kujikwamua katika maisha yao ya kila siku na sio muda mwingi kulalamika na kukaa bila kujishughulisha.

Akizungumzia juu ya suala la elimu, Msongozi alisema kuwa watoto wote waliomaliza darasa la saba mwaka huu, wazazi wao wahakikishe wanawapeleka shule kwa ajili ya kuanza kidato cha kwanza na sio kuwaacha nyumbani au mitaani wakiwa wanazurula hovyo na kujifunza matendo maovu kama vile uvutaji wa madawa ya kulevya.

“Ndugu zangu ona fahari kuona kwamba, mtoto wako anapata elimu na sio kumtumikisha kwa kufanya kazi za kuchunga ng’ombe au mbuzi tuone kwamba ni wajibu wetu watoto hawa, mwisho wa siku wanakuwa na elimu ya kutosha”, alisema.

No comments: