Thursday, December 24, 2015

SEKONDARI MAHANJE WANAFUNZI KUKOSA MADARASA YA KUSOMEA



Na Muhidin Amri,
Songea.

SHULE ya sekondari Mahanje iliyopo katika kata ya Mahanje wilayani Songea mkoa wa Ruvuma, inakabiliwa na uhaba mkubwa wa vyumba vya madarasa jambo ambalo linatishia watoto walioteuliwa kuanza kidato cha kwanza kwa mwaka wa masomo 2016, kukosa  mahali pa kusomea.

Kwa sasa shule hiyo ina vyumba  vinne vya madarasa kati ya 10 ambavyo vinahitajika ili viweze kutosheleza wanafunzi watakaoingia shuleni hapo kwa ajili ya kuanza masomo ya kidato cha kwanza hadi cha nne.

Aidha kutokana na hali hiyo, baadhi ya wadau wameanza kujitokeza akiwemo Mbunge wa jimbo la Madaba Joseph Mhagama aliyetoa bati 130 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa, katika shule hiyo.


Mbunge huyo amewataka wakazi wa  jimbo hilo, kujitokeza kwa wingi kuchangia nguvu zao ili kuweza kukamilisha ujenzi wa vyumba hivyo madarasa.

Ametoa wito kwa kamati ya shule sekondari Mahanje, walimu na baadhi ya watumishi wa Halmashauri hiyo kujenga ushirikiano wa pamoja kwa kuhimiza pia wananchi kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo jimboni humo.

Vilevile alibainisha kuwa kuna baadhi ya vijiji ambavyo vimekosa maendeleo kwa sababu wananchi wake, kutofanya kazi kwa bidii na  hata kuchangia shughuli za maendeleo katika jamii.

Licha ya jimbo hilo kuwa  na ardhi kubwa inayofaa kwa  kilimo cha mazao mbalimbali, alisema kuwa bado kuna baadhi ya watu wanakabiliwa na umaskini unaotokana na kutofanya kazi za kujiongezea kipato na ndiyo maana wengine wanashindwa kumudu hata  mlo  mmoja kwa siku, kutokana  na uvivu walionao.

Mhagama aliongeza kuwa, muda wa kuzungumzia mambo ya siasa umekwisha na kilichobaki sasa wananchi wanapaswa kuungana na viongozi wao kufanya kazi za  mendeleo, chini ya kauli mbiu ya ‘hapa kazi tu’, badala ya  kutumia muda wao kukaa vijiweni na kufanya starehe ambazo zinawagharimu katika maisha yao.

Kwa mujibu wa  Mbunge huyo ni kwamba, dawa ya kumaliza umaskini wanayo wananchi wenyewe kwani wanachotakiwa kufanya ni kujituma kwa moyo  mmoja na kujikita zaidi kufanya kazi kwa kushirikiana na watendaji na madiwani wao katika kuibua na kutekeleza miradi, kwenye maeneo yao ambayo itawawezesha kupata huduma bora katika maeneo yao.

No comments: