Sunday, December 27, 2015

WAZAZI WATAKIWA KULEA WATOTO WAO KATIKA MISINGI YA MAADILI MEMA



Na Julius Konala,
Songea.

ZAIDI ya watoto 300 wamebatizwa Jumapili ya sherehe za krismasi kwenye Kanisa katoliki Parokia ya Bombambili, Jimbo kuu la Songea mkoani Ruvuma kitendo ambacho kimeelezwa kuwa ni cha kihistoria kwa madai kwamba, ni mara ya kwanza kutokea tangu kuanzishwa kwa Parokia hiyo.

Ibada hiyo ya misa takatifu ya ubatizo iliongozwa na Padri Godfrey Nchimbi, huku akisaidiwa na mapadre wengine mbalimbali wakiwemo Otieno Olwen na Simon Ndunguru ambaye ni Paroko wa parokia hiyo ya Bombambili.

Sambamba na hilo jumla ya watu 73 walipata sakramenti ya ndoa katika kanisa hilo, tukio ambalo lilitanguliwa na baadhi yao ambao hawakuweza kufuata hatua za sakramenti kwa kufuata utaratibu wa kanisa, walianza kupewa sakramenti ya ubatizo, kipaimara na kisha kufungishwa ndoa.

Matukio hayo yote mawili yalikwenda sambamba na kula chakula cha pamoja kilichoandaliwa na Paroko wa parokia hiyo, Padri Simon Ndunguru katika ukumbi wa mikutano wa parokia hiyo na kuhudhuriwa na waumini mbalimbali, wakiwemo wasimamizi wa watoto wa ubatizo na ndoa.


Awali akihubiri katika ibada hiyo ya misa takatifu ya ubatizo na ndoa, Padri Otieno Olwen amewataka wazazi kuwalea watoto wao katika misingi ya maadili mema ili kanisa na taifa kwa ujumla, liweze kupata viongozi waadilifu.

Olwen alisema kuwa ufisadi, wizi na vitendo vingine viovu ni matokeo ya wazazi kushindwa kuwalea watoto wao katika misingi ya uadilifu ambapo amewataka wazazi na walezi wa watoto hao, kuhakikisha wanawafundisha kufuata imani ya dini yao kwa kuhudhuria na kushiriki ibada mbalimbali.

Akizungumzia kwa upande wa wanandoa aliwataka kudumisha na kuheshimu ndoa zao, badala ya kusikiliza maneno ya watu wa nje ambao wanaongea uongo na kuchonganisha kwa malengo ya kuzifarakanisha huku akiwaasa kuheshimiana na kuombana msamaha pindi wanapokorofishana.

No comments: