Monday, December 14, 2015

MWAMBUNGU ATUMBUA JIPU BARAZA LA MADIWANI HALMASHAURI YA MJI WA MBINGA



Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

SERIKALI mkoani Ruvuma, imesema Diwani anayefikiri ameingia madarakani kwa lengo la kupata utajiri ni vyema ajiondoe mapema, kwani haitaweza kumvumilia mtu wa namna hiyo na endapo atabainika mwisho wa siku atachukuliwa hatua na kuondolewa madarakani. 

Aidha imefafanuliwa kuwa wengi wao waliongia madarakani kupitia cheo cha udiwani, wanafikiri ndio njia pekee ya kuendekeza vitendo vya rushwa na ufisadi katika kuhujumu miradi ya wananchi, kwa lengo la kujinufaisha wao binafsi.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu alitoa rai hiyo leo alipokuwa akihutubia baraza la kwanza la Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani humo, ambalo liliketi katika ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.
Said Mwambungu, Mkuu wa mkoa wa Ruvuma.

Mwambungu alikuwa akiwasilisha salamu za serikali katika baraza hilo, ambapo aliwataka pia Watendaji wa serikali kushirikiana pamoja na madiwani hao ili kuweza kufikia malengo ya kimaendeleo, yaliyokusudiwa kwa manufaa ya jamii.

“Ndugu zangu kiongozi ambaye ni mpenda rushwa au fisadi aliyekubuhu, tukikubaini tutakuchukulia hatua na mwisho wa siku tutakuondoa, tafuteni maisha kwa njia zilizohalali acheni kujihusisha na matendo maovu”, alisisitiza Mwambungu.

Alieleza kuwa ili Halmashauri ya mji huo na mkoa wa Ruvuma kwa ujumla, uweze kupiga hatua mbele ya kimaendeleo, viongozi wanawajibu wa kudhamiria kuwatendea haki wananchi ili mwisho wa siku jamii iwakumbukwe kwa mema na sio mabaya.


“Hapa na maanisha kwamba kila ngazi itekeleze wajibu wake, mapato yatumike kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa, hatutamsamehe wala kujenga huruma kwa mtu ambaye ni mwizi, na mwenye lengo la kutaka kuturudisha nyuma kimaendeleo”, alisema.

Kadhalika Mkuu huyo wa mkoa aliongeza kuwa, lengo la serikali ni kutaka kwenda na kasi ambayo inaendana na weledi, uaminifu na uadilifu wa hali ya juu katika utendaji kazi kwani wakati nchi hii inapata Uhuru, Hayati Mwalimu Julius Nyerere alisema kila mtu ni lazima afanye kazi kwa faida ya Taifa hili.

Vilevile Mwambungu hakuwa mbali kwa kuwataka viongozi na wananchi kwa ujumla, kuzingatia masuala ya usafi katika maeneo yao wanayoishi na kwamba Ofisi yake hapa mkoani Ruvuma, imejiwekea utaratibu kwamba kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi ni siku ya kusafisha mazingira.

Awali kabla ya Mkuu huyo wa mkoa kutoa salamu hizo kwa baraza hilo la Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga, ulifanyika uchaguzi wa kumpata Mwenyekiti, Makamu wake na kamati mbalimbali za halmashauri hiyo.

Kwa nafasi ya Mwenyekiti ilichukuliwa na diwani wa kata ya Myangayanga, Ndunguru Kipwele kutoka tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) aliyepata kura (24) huku akimbwaga chini mpinzani wake wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Frank Mgeni kutoka kata ya Mbinga mjini ‘B’ kwa kupata kura 2.

Nafasi ya makamu Mwenyekiti ilinyakuliwa na wa CCM kutoka kata ya Kikolo, Tasilo Ndunguru aliyepata kura 23 na kumwacha mbali mgombea mwenzake wa CHADEMA, Aidan Nombo wa kata ya Utiri kwa kura 3.

No comments: