Thursday, December 10, 2015

TUNDURU NAKO WATEKELEZA ZOEZI LA USAFI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MAELFU ya Wananchi katika wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, wamepongeza maamuzi ya serikali ya awamu ya tano, kufanya maadhimisho ya sherehe za miaka 54 ya Uhuru kwa kufanya usafi, jambo ambalo Watanzania linawakumbusha kuwa ni wamoja.

Hayo yalibainishwa na wananchi hao kwa nyakati tofauti, walipokuwa wakizungumza na mwandishi wetu wakati walipokuwa wakishiriki katika zoezi la kufanya usafi kwenye maeneo yao, kwa lengo la kuweka mazingira yao katika hali ya usafi ili kuweza kupambana na adui maradhi.

Miongoni mwa waliopata nafasi ya kuzungumzia tukio hilo, ni pamoja na mtendaji wa kata ya  Nakayaya wilayani humo, Zainabu Issa ambaye alikutwa akiwa na timu yake wakifanya usafi katika eneo la kata hiyo.


Alisema kuwa awali wananchi wengi walijenga dhana kwamba, jambo la usafi katika maeneo ya mijini au masoko ni jukumu la serikali pekee lakini baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Magufuli kuonesha njia kila mtu ameanza kutambua kuwa usafi ni wajibu wa kila mtu.

Wengine ni fundi mkuu wa mitambo katika viwanda vya kubangulia korosho wilaya ya Tunduru, Masasi, Newala na Mtwara Mhandisi Sivan Edayeth ambaye alisema kwamba usafi wa mazingira katika maeneo tunayoishi ni jukumu la kila mtu ili kuweza kuepukana na wadudu ambao huleta magonjwa mbalimbali.

Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Agnes Hokororo ambaye aliwaongoza mamia ya watumishi wa idara ya serikali katika zoezi hilo kwenye maeneo ya ofisi za Boma, Halmashauri, Hospitali ya Wilaya na kuhitimisha shughuli hiyo katika eneo la soko kuu la Azimio alisema usafi wa mazingira katika maeneo yao yatakuwa endelevu.

Naye Mkurugenzi mtendaji wa Hamashauri ya wilaya ya Tunduru, Tina Sekambo alisema kuanzia sasa hakuna mtu, atakaye vumiliwa endapo atapuuzia agizo la kufanya usafi katika eneo lake.

No comments: