Wednesday, December 23, 2015

UKOSEFU WA FEDHA WAKWAMISHA MAENDELEO MBIUWASA



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEBAINIKA kuwa, Mamlaka ya maji safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, inashindwa kutimiza mahitaji halisi ya utoaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wateja waliopo katika mji huo, kutokana na miundombinu iliyopo kuwa chakavu.

Vilevile uzalishaji wa maji safi na salama kwa sasa katika mji huo ni mita za ujazo 2,100 kwa siku, ikilinganishwa na mahitaji halisi yanayotakiwa kuzalishwa ni mita za ujazo 3,640 kwa siku ambapo Mamlaka hiyo inashindwa kufikia malengo hayo, kutokana na tatizo hilo linalowakabili.

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wetu umebaini kuwa mji wa Mbinga, una wakazi 43,674 kati ya hao wakazi 26,204 wanaishi katika eneo lilipopita bomba la usambazaji maji huku maeneo mengine yaliyo pembezoni mwa mji, yakiwa hayana mtandao wa maji safi na salama.


Mji huo kwa sasa ambao unakua kwa kasi kiuchumi na ongezeko la watu likizidi kukua, idadi ya wateja wanaopata maji hayo hivi sasa ni 2,075 kiasi ambacho ni kidogo, tofauti na idadi halisi ya wakazi wanaoishi katika mji huo.

Katika kuleta ufanisi mzuri wa utoaji wa huduma hiyo kwa walaji na utekelezaji wa kazi za kila siku za MBIUWASA, kuna kila sababu kwa mamlaka hiyo kufanya marekebisho ya bei za maji ikiwemo kupandisha bei za huduma ili iweze kukusanya mapato ya kutosha, yatakayoweza pia kumudu gharama za uendeshaji na uboreshaji wa miundombinu husika ili huduma ya maji iweze kuwafikia idadi kubwa ya wananchi ipasavyo.

Meneja wa Mamlaka hiyo, Patrick Ndunguru alipotakiwa kutoa ufafanuzi juu ya hali hiyo alithibitisha hilo na kueleza kuwa hali ya ukusanyaji mdogo wa mapato yatokanayo na maji, kunasababisha washindwe kupeleka huduma ya maji maeneo yasiyofikiwa na mtandao wa bomba kutokana na mji kukua kwa kasi ikilinganishwa na kasi ya upelekaji huduma.

Alisema kuwa tatizo jingine linalowakabili kushindwa kukarabati mabomba ambayo mengi kwa sasa ni chakavu, huvuja na kupoteza maji kwa wingi pamoja na kushindwa kubadilisha dira za maji zilizokwisha muda wake wa matumizi jambo ambalo linasababisha zishindwe kufanya kazi na kuisababishia taasisi hiyo hasara.

“Tunashindwa hata kupandisha kiwango cha mishahara kwa watumishi wetu wa mamlaka na kulipa madeni kwa wakati, kwa wazabuni wetu ambao hutusambazia vifaa kwa ajili ya kuboresha huduma ya usambazaji maji katika mji wa Mbinga”, alisema Ndunguru.

Ndunguru alisema kuwa, endapo bei za maji hazitarekebishwa athari yake ni kwamba huduma zitaendelea kudorola kadiri siku zinavyozidi kusonga mbele hivyo Mamlaka ya maji safi na Usafi wa Mazingira katika mji wa Mbinga, hivi karibuni ilishirikisha Wadau husika wa mji huo kwa kufanya mkutano na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) na kwamba michakato ya kuliweka sawa jambo hilo, inaendelea ili jamii hapo baadaye iweze kupata huduma bora ya maji safi na salama na kuepukana na athari mbalimbali.

No comments: